Rais mstaafu wa awamu ya tatu, Benjamin Mkapa, amesema changamoto iliyopo nchini ni kuanzishwa kwa vyuo vikuu vitakavyotoa mafunzo maalum yanayojumuisha makundi mbalimbali ya wanajamii, wakiwemo watu wenye ulemavu na wanyonge.habari zaidi...
Alisema kuna haja hiyo kwa kuwa mahitaji ya elimu ya juu katika soko la ajira yanazidi kuongezeka kutokana na maendeleo makubwa ya sayansi na teknologia duniani.
Alisema hayo juzi wakati akihutubia sherehe za mahafali ya kwanza ya Chuo Kikuu cha Sebastian Kolowa (Sekuco) kilichopo wilayani hapa mkoa wa Tanga, ambapo wanafunzi 135 walihitimu Shahada katika fani ya elimu maalum na kutunukiwa vyeti na Mkuu wa Chuo Kikuu cha Tumaini ambaye pia ni kiongozi wa Kanisa la Kiinjili la Kilutheri Tanzania (KKKT), Askofu Dk. Alex Malasusa.
Rais huyo mstaafu alisema uanzishwaji wa chuo kama Sekuco ni moja ya njia za kujenga jamii jumuishi, inayothamini utu, haki, na uwezo wa kila binadamu, wakiwemo walemavu wa aina mbalimbali.
Mkapa alisema kuwa chuo hicho ni mfano wa kuigwa kwa kuwa Tanzania inahitaji wataalamu katika fani zenye vipaji mbalimbali zitakazokidhi mahitaji ya watu wa makundi yote katika jamii.
Aliwataka waahitimu kutumia taaluma waliyoipata kama ukombozi kwa makundi maalum, na kufafanua kuwa ulimwengu wa sasa unahitaji wasomi wenye upeo wa juu katika fani zao, wenye kuelewa mambo, kuchambua na kutatua matatizo katika jamii, huku akisisitiza kuwa enzi ya kukariri imepitwa na wakati.
“Msije mkatumia ujuzi wenu mlioupata hapa kugushi, kula rushwa, ama kutumia mbinu chafu za kujipatia kipato kwa njia zisizokubalika kimaadili ya Tanzania ya taaluma yenu…utumishi bora unadai mjiepushe na kauli ya ‘njoo kesho,” alisema Mkapa.