Mashirika ya misaada yametoa wito wa kufanyika kwa juhudi za kuzuia mauaji yanayofanywa na kundi la waasi linaloogopwa zaidi barani Afrika, katika kipindi hiki cha Krismasi.Wapiganaji wa LRA waliua mamia ya watu katika Jamhuri ya Kidemokrasi ya Kongo (DRC) na Sudan mwezi Disemba mwaka 2008 na 2009.

Kundi hatari

Mamia ya watu walitekwa katika kipindi hicho cha mashambulio.
Takwimu zinaonesha kuwa kundi la LRA katika kipindi cha miaka miwili iliyopita, limekuwa ndio kundi hatari zaidi katika Jamhuri ya Kidemokrasi ya Kongo, yamesema makundi hayo katika ripoti yao.
Katika siku ya Krismasi mwaka 2008, na wiki tatu zilizofuatia, LRA iliwapiga hadi kuwaua zaidi ya watu 800 kaskazini-mashariki mwa DRC na Sudan Kusini, na kuteka mamia wengine.
Mwezi Disemba mwaka 2009, kundi hilo liliua zaidi ya wanavijiji 300 nchini DRC katika siku kadhaa karibu na Krismasi.
Msemaji wa LRA amekanusha kuwa kundi lake lilihusika na mauaji hayo.
Waasi hao ambao asili yao ni Uganda, pia wanarandaranda katika maeneo ya Sudan na Jamhuri ya Afrika ya Kati waliua au kuteka nyara zaidi ya watu 1,000 katika maeneo ya vijijini ya DRC mwaka jana pekee, imesema ripoti hiyo.
Mashirika hayo yamesema juhudi za pamoja zinahitajika kuzuia kundi hilo la Lords Resistance Army (LRA) kufanya mauaji ambayo sasa yanajulikana kama "mauaji ya Krismasi".