Mshambuliaji kutoka Cameroon, Samuel Eto'o, amekuwa mtu wa kwanza kushinda tuzo ya mwanasoka bora wa Afrika wa Mwaka, kwa mara ya nne.
Tuzo hiyo ya Eto'o kwa mara ya nne, ameweza sasa kuwapiku waliowahi kushinda mara tatu barani Afrika, Abedi Pele na George Weah.
Katika sherehe ya kukabidhiwa tuzo hiyo mjini Cairo, Eto'o alisema: "Nina furaha kushinda kwa mara nyingine, kuweza kupata tuzo hii mara ya nne dhidi ya wachezaji wengine hodari."
"Afrika ina wachezaji wengi wazuri na kuna vipaji vingi vinachipuka, kwa hiyo nadhani hii itakuwa nafasi yangu ya mwisho." Aliongeza Eto'o
Eto'o amekuwa mhimili wa mafanikio ya klabu ya Inter Milan msimu uliopita, ambapo alipachika mabao 16 chini ya kocha Jose Mourinho.
Hata hivyo mchango wake haukuwa mkubwa kwa timu yake ya taifa ya Cameroon, baada ya kutolewa mapema katika mashindano ya kuwania Kombe la Mataifa ya Afrika nchini Angola na Kombe la Dunia nchini Afrika Kusini.