Idhaa ya BBC ya World Service imetangaza mipango yake ya kufunga idhaa tano zinazotangaza kwa lugha mbali mbali- Kiserbia, Albania, Macedonia, Kireno kwa Afrika pamoja na idhaa inayotangaza kwa lugha ya Kiingereza huko Caribbean.(Pichani watangazaji wa idhaa ya kiswahili kushoto ni Charles Hilary na Salim kikeke.)

Inakadiriwa idadi ya wasikilizaji itapungua kwa zaidi ya milioni 30 kutoka wasikilizaji milioni 180 wa sasa.
Mkurugenzi mkuu wa BBC Mark Thomson, amesema kufungwa kwa idhaa hizo kutakuwa na athari kubwa kwa wasikilizaji wanaotegemea kupata manufaa mbali mbali.
Mkurugenzi mkuu wa BBC World Service, Peter Horrocks, amesema hatua hii inafuatia mpango wa serikali wa kupunguza ufadhili wake. Hata hivyo ameongezea kuwa bado atahakikisha BBC World Service itabakia kwenye nafasi ya juu katika kutoa habari.
Hatua hii ya BBC imeshutumiwa na Muungano wa Kitaifa wa waandishi wa habari (NUJ).
BBC World Service itasitisha matangazo yake kupitia ShortWave katika idhaa zingine sita ifikapo mwezi Machi, 2011 zikiwemo - Hindi, Indonesian, Kyrgyz, Nepali, Kiswahili pamoja na Maziwa Makuu.Ingawa matangazo ya Idhaa ya Kiswahili ya BBC kupitia Shot Wave yatasitishwa, tayari kuna ushirikiano wa idhaa hiyo na mashirika mengine ya utangazaji kupitia vipimo vya FM.

Mipango ya sasa ni kuangazia zaidi ushirikiano kama huu pamoja na kupeperusha matangazo yake kupitia kwa mtandao na simu.
Pia kuna mipango ya kuanza kushirikiana na vituo vya televisheni kupeperusha matangazo ya Idhaa ya Kiswahili ya BBC.