MSANII wa muziki wa kizazi kipya, Ummy Wenceslaus ‘Dokii’ ametunga nyimbo
zinazohamasisha suala la Polisi Jamii na Ulinzi shirikishi.

Akizungumza na waandishi wa habari katika kituo cha Polisi Kati Dar es Salaam jana Dokii alisema hivi sasa yuko kwenye mchakato wa kuandaa albamu juu ya suala hilo ambapo anaamini itatoa somo kwa jamii.
 “Nimevutiwa sana na kazi ya Kamanda wa Polisi Kanda Maalumu ya Dar es Salaam, Suleiman Kova na kuona anahitaji kuungwa mkono na jamii nzima inayomzunguka ikiwa wananchi na wanamichezo wote”.

Alisema wimbo wake ya kwanza unaoitwa Kombe la Kova, atauzindua siku itakayoanza michuano hiyo ambapo ndipo atakapoizindua pia albamu hiyo.

“Nimeelezea kwamba wananchi na wanamichezo imefika kipindi tuungane na kuhamasisha wananchi kutoa taarifa za wahalifu katika vyombo vya Polisi,” alisema Dokii.

Naye Kamanda Kova, amempongeza Dokii kwa ujasiri huo na kuwataka mabondia, wananchi, waimbaji kushirikiana na Polisi ili kuweza kutokomeza uhalifu.

“Wahalifu ni miongoni mwa watu ambao tunaishi nao mitaani, hivyo wote tukiamua kushirikiana basi jambo hili litafika mwisho,” alisema Kamanda Kova.