KAULI ya Bodi ya Filamu ya kupiga marufuku majina ya filamu yenye lugha ya kigeni imepokewa kwa hisia tofauti na watengeneza sinema ambao wamesema Bodi haistahili kuwatisha ila kuwasaidia.

Kauli hiyo imetolewa na Steven Kanumba jana katika mkutano na waandishi wa habari kwenye ofisi za Kampuni ya kusambaza sinema ya Steps Entertainment.

Mkutano huo ulitumika kumkabidhi Kanumba tuzo ya filamu bora inayokwenda Fespaco, Burkinafaso ya This is it na Hanifa Daud ‘Jenifer’ tuzo ya muigizaji bora chipukizi aliyoipata kupitia filamu hiyo.

Tuzo hizo zilitolewa karibuni mjini Zanzibar na tamasha la Filamu la kimataifa la Zanzibar, ZIFF, ambalo liliendesha tamasha dogo kwa lengo la kupata filamu bora mbili nchini zitakazowakilisha taifa nchini Burkinafaso katika tamasha la filamu la Fespaco.