Uvamizi wa anga unaofanywa na majeshi ya muungano umeshambulia eneo alipozaliwa Kanali Muammar Gaddafi huko Sirte, eneo muhimu linalolengwa na waasi lililopo upande wa magharibi.
Msemaji wa serikali ya Libya alisema raia watatu wa Libya waliuliwa kwenye bandari ya nchi hiyo.
Uvumi ambao haukuthibitishwa kuwa waasi waliudhibiti mji wa Sirte ulisababisha waasi kufyatua risasi kwa minajil ya kushangilia kwenye mji walioukhodhi wa Benghazi.

Waandishi wa kigeni Sirte walisema walisikia milipuko mikubwa kwenye mji huo huku ndege zikipita angani.
Msemaji wa waasi huko Benghazi alisema Sirte sasa ilikuwa mikononi mwa majeshi ya waasi- lakini hakujakuwa na uthibitisho binafsi kutokana na madai hayo, na waandishi wa habari wa kimataifa ndani ya mji huo walisema bado unadhibitiwa na serikali.
Wakati huo huo, Qatar ni taifa la kwanza la kiarabu kutambua uongozi wa waasi- Baraza la Taifa la Mpito- kama wawakilishi rasmi wa watu wa Libya.