Waziri Mkuu wa Uturuki, Recep Tayyip Erdogan, ametoa matamshi makali dhidi ya Rais Bashar Assad wa Syria.
Bw Erdogan amesema hakuna utawala utakaodumu kwa kuwaua na kuwafunga wapinzani wake, akisema Syria ya baadaye haiwezi kujengwa kwa kumwaga damu ya raia wanaokandamizwa.
Amesema haya wakati mawaziri wa mambo ya nje kutoka Jumuiya ya Ulaya wakikutana hii leo mjini Rabat Morocco.
Kikao cha leo kinatarajiwa kuongeza shinikizo dhidi ya Syria kufuatia harakati za majeshi yake dhidi ya waandamanaji.
Makundi ya kutetea haki za kibinadamu yamesema raia 70 wameuawa katika machafuko ya hivi karibuni.
Naye katibu mkuu wa Umoja wa mataifa ameitaka jumuiya ya nchi za Kiarabu kuwa na msimamo moja dhidi ya utawala wa Damascus.
Marekani kwa upande wake imetaka ujumbe mkali kutumwa kwa Syria.

Uturuki ambayo ni jirani ya Syria aidha imetishia kukatiza huduma ya umeme inayotoa kwa Syria. Na katika juhudi za kupunguza ghathabu ya kimataifa, Syria imeachia huru wafungwa elfu moja wa kisiasa.
Hata hivyo, Damscus ilipata jibu kali pale mfalme wa Jordan alipomtaka Rais Assad kuachia madaraka. Mfalme huyo amesema matukio ya sasa hayampi Bashar Al Assad uhalali wa kuendelea kuongoza nchi hiyo.