Jeshi la Tanzania limesema limewakamata wanajeshi 20 waliokuwa wamejihami vikali kutoka nchi jirani ya Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo.

Msemaji wa jeshi la Tanzania katika mji wa Magharibi wa Kigoma, amesema wanajeshi hao wa Congo waliingia nchini humo kinyume cha sheria, wakitumia boti, baada ya kuwafukuza wapiganaji wa waasi katika ziwa Tanganyika.

Ripoti zinasema kuwa wapiganaji hao walikuwa wamejihami na bunduki za rashasha, maguruneti yanayorushwa kwa kutumia roketi na kiasi kikubwa cha risasi.

Idadi kubwa ya wapiganaji wa waasi kutoka Congo, waliwasili mjini Kigoma siku ya Alhamisi, kutafuta matibabu. Wengi wao walikuwa na majeraha mabaya ya risasi.