NDOA ya kifahari iliyofungwa kwa mbwembwe nyingi na kuweka rekodi ya aina yake kwa mastaa wa sinema za Kibongo kati ya Irene Pancras Uwoya (pichani) na msukuma kabumbu wa Kimataifa wa Rwanda, Hamad Ndikumana ‘Kataut’ imevunjika, Risasi Mchanganyiko lina ushahidi mkononi.

Kwa mujibu wa chanzo chetu halali, ndoa hiyo imepinduka usiku wa Jumapili kufuatia kushindwa kuvumiliana kama walivyoahidiana siku ya kufungwa kwa ndoa hiyo.

SIMU YA MTOA HABARI YAINGIA
“Mambo vipi? Sikieni, Ndoa ya Irene Uwoya na Ndikumana imevunjika, mna habari hiyo? Hivi ninavyowaambia, Irene hayuko kwake, Ndikumana hajui aanzie wapi,” kilisema chanzo hicho kwa sauti iliyojaa masikitiko.

Baada ya kutoa habari hizo, chanzo kikakata simu kikiamini kama kuna maswali kitapigiwa kwa vile namba zake ziko kwenye dawati la gazeti hili.

RISASI LAMSAKA UWOYA KUPATA UKWELI
Kufuatia madai hayo mazito, paparazi wetu Imelda Mtema alimtwangia simu Uwoya na kumuuliza alipo.

Uwoya: Nipo Mbezi, huku Kawe kwani vipi Ime?

Imelda: Mbezi kwenye nini, nataka kuja kuna ishu nimeisikia kuhusu wewe.
Uwoya: Mh! Ishu gani hiyo Ime? Anyway njoo.

Uwoya alimwelekeza mwandishi alipokuwa, baada ya robo saa, Imelda alifika huku akitegemea kumuona msanii huyo analia au yupo katika uso wenye wakati mgumu, lakini ikawa kinyume.

Uwoya: (huku akitabasamu) Imelda kuna nini jamani?

Imelda: Irene, tofauti na ulivyo, lakini kuna habari zimetua ofisini kwamba umeachana na mumeo, Ndikumana, kuna ukweli wowote?

Katika hali ambayo haikutarajiwa, Irene bila kuuma maneno wala kupoteza muda, alikiri kuachana na Ndikumana. Maskini wee!
Imelda: Ha! Kisa nini lakini?

Uwoya: Hakuna kisa cha moja kwa moja, lakini sikuwahi kuwa na furaha katika maisha yangu ya ndoa na yeye.

Imelda: Hukuwahi kuwa na furaha? Mbona unaonekana uko sawa hata uso umezidi kupendeza?

Uwoya: Mimi ndiye ninayejua, kwanza sijawahi kumpenda Ndikumana kabla sijafunga naye ndoa na hata baada ya kufunga.

Imelda: Sasa kama ulikuwa humpendi uliwezaje kufunga naye ndoa Irene, tena ya kifahari?



Uwoya: Ime, ile ndoa kama nililazimishwa lakini sikuwa na mapenzi ya dhati.

Kwanza wiki moja kabla nilitaka kuondoka Dar, mama akanizuia akisema nitamuaibisha.


Imelda: Sasa kama ni kweli umeachana na Ndikumana nini matarajio yako?

Uwoya: Kiukweli Imelda nina mtu ambaye nampenda sana, hisia zangu ziko kwake.

Imelda: Looo! Huoni kama jamii itakuchukulia tofauti Irene?

Uwoya: Najua watasema sana, lakini sijali kwa vile mimi ndiye ninayepata tabu kuishi na mtu nisiyempenda.

Imelda: Juzikati ilidaiwa alikupiga, au ndiyo sababu?

Uwoya: Hata asingenipiga, kuachana kulikuwa njiani.

Hata hivyo, nimejitahidi sana kuishi naye miaka miwili na nusu! (Miezi 18)
Imelda: Wazazi wako wanajua?

Uwoya: (akiinamisha kichwa) mama amesema hataki kusikia, lakini mimi ndiye mwenye maamuzi ‘coz’ (kwa sababu) ndiye niliyeishi naye.

Imelda: Ndikumana mwenyewe anasemaje kuhusu uamuzi wako?

Uwoya: (Akiachia tabasamu) aseme nini sasa? Toka zamani nilikuwa nikimwambia sina mapenzi ya kweli na yeye, kwa hiyo alilijua hilo.

Imelda: Sasa huku baa, tena baharini umefuata nini?

Uwoya: (Anakunja sura) nahitaji kuwa peke yangu zaidi nikitafakari ya baadaye.

Imelda: Vipi kuhusu hatima ya mtoto wenu, Krish?

Uwoya: (Akionekana kuumia usoni) yupo kwa bibi yake.

KUMBUKUMBU YA NDOA
Irene na Ndikumana walifunga ndoa Julai 11, 2009 katika Kanisa la Mtakatifu Joseph na kufuatiwa na sherehe ya kufa mtu kwenye Hoteli ya Giraffe View, iliyopo Mbezi Kawe, jijini Dar es Salaam.

Harusi hiyo ilidaiwa kugharimu kiasi cha shilingi 80,000,000 za Kitanzania huku baadhi ya vyombo vya habari vikiichambua kuwa ndiyo harusi kubwa kuliko za mastaa wengine Bongo.

NDOA YACHELEWA KUJIBU
Maisha ya ndoa ya wawili hao yalikuwa Cyprus, jijini Nicosia ambalo ndiyo mji mkuu wa nchi hiyo. Ndikumana aliajiriwa kucheza mpira kwenye Klabu ya AEL Limassol na baadaye Apop Kinyras Peyias FC.

Mei 8, 2010, Uwoya alijifungua mtoto wa kiume (Krish) katika Hospitali ya Regency, Upanga, Dar, hivyo kuandika historia nyingine katika ndoa yake.

KUMBUKUMBU ZENYE UKWELI?
Tangu aolewe, kwenda kuishi kwa mumewe Cyprus, Uwoya amekuwa akipamba magazeti pendwa kwa vichwa vya habari vyenye madai, maonyo na maelekezo kutokana na tabia yake ya kurudi Bongo kila wakati.

Mfano; NENDA RUDI YA UWOYA KWA MUMEWE YAZUA MASWALI, …UWOYA ARUDI KWAO, UWOYA LAIVU (alikuwa amekumbatiana na mwanaume akiwa ni mke wa mtu), na vingine vingi.Jitihada za kumpata Ndikumana kwenye simu ili azungumzie kile anachokijua hazikuzaa matunda siku ya Jumatatu jioni baada ya simu yake ya kiganjani kuita kwa muda mrefu bila kupokelewa.

Mwandishi wetu alikwenda nyumbani kwa mama wa Uwoya, lakini msichana aliyekuwa hapo alisema mama Irene hakuwepo bila kufafanua alipokwenda.