(John Terry siku alipokwaruzana na Anton Ferdinand)

Nahodha wa England John Terry amehojiwa na polisi kuhusiana na tuhuma alimtolea maneno ya ubaguzi Anton Ferdinand.
Terry, mwenye umri wa miaka 30, ambaye pia ni nahodha wa Chelsea, anakanusha kumtolea maneno ya kibaguzi mchezaji huyo wa QPR wakati wa mchezo wa tarehe 23 mwezi wa Oktoba.
Polisi wamethibitisha "mtu mwenye umri wa miaka 30 amehojiwa tarehe 25 mwezi wa Novemba. Hajakamatwa."
Chama cha Kandanda cha England -FA- kwa upande wake kinachunguza suala hilo.
Baadhi ya watu wamedai mkanda wa video uliorudiwa baada ya mechi iliyochezwa uwanja wa Loftus Road Terry alionekana akitumia lugha ya kibaguzi, wakati FA ilisema ilipokea malalamiko hayo.
Ferdinand awali alitoa taarifa kwa FA, akisema "analitilia maanani sana" suala hilo, lakini hatafafanua hadi uchunguzi wa FA utakapokamilika.
Uchunguzi wa FA kuhusiana na suala hilo hautatolewa hadi polisi watakapokamilisha uchunguzi wao.
Katika taarifa baada ya mechi ya Loftus Road, Terry alielezea tukio hilo kama ni "kutoeleweka" na akadai anayemtuhumu "alifika hatua ya mwisho ya suala hilo kwa makosa juu ya muktadha wa kile ambacho nimeonekana nikikisema".
Aliongeza: "Kamwe siwezi kusema kitu kama kama hicho - Nimeshangaa watu kufikiria kama naweza kutamka hayo."