HIVI karibuni, Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Dk. Mohamed Shein, alizungumza na wahariri wa vyombo vya habari mbalimbali nchini mjini Zanzibar ambapo, pamoja na mambo mengine, alizungumzia lawama zinazoelekezwa kwake kwa kula kiapo kuwa mmoja wa wajumbe wa Baraza la Mawaziri la Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, kwamba inadhalilisha hadhi na nafasi ya Rais wa Zanzibar na Serikali ya Watu wa Zanzibar kwa ujumla.
Akionekana dhahiri kukerwa na lawama hizo, kwa sauti ya ukali na ghadhabu kubwa, Dk. Shein alisema: “Nilipoapishwa kuwa Rais wa Zanzibar, niliapa kuilinda Katiba (ya Muungano) na nitailinda kwa nguvu zangu zote nikiwa kiongozi.”
Alifafanua kuwa, Rais wa Zanzibar anaingia kwenye baraza hilo kulinda maslahi ya Zanzibar katika Muungano na anabaki Rais wa Zanzibar si kama waziri asiyekuwa na wizara maalumu wanavyomtuhumu Wazanzibari:
“Mbona mimi siyo wa kwanza kuapa….Amani Abeid Karume (mstaafu) alifanya hivyo, tena mara mbili (2000 na 2006) na mimi nilishuhudia na hakukuwa na malalamiko; iweje kwangu miye?” alihoji Dk. Shein.
Ibara ya 54 (1) ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano ya 1977 inatamka: “Kutakuwa na Baraza la Mawaziri ambalo Wajumbe wake watakuwa ni Makamu wa Rais, Waziri Mkuu, Rais wa Zanzibar na Mawaziri wote”.
Wasomaji wangu na wale Wazanzibari (wachache?) wanaomtuhumu Dk. Shein kwa kitendo hicho, bila ya kupatiwa ufafanuzi makini, wanaweza kuendelea kuhoji kupata majibu ya maswali kama: Je, ni sahihi kwa Rais wa Zanzibar kula kiapo cha uwaziri chini ya Katiba ya sasa ya Muungano? Je, viapo vya Rais wa Zanzibar aliyemtangulia vinaweza kuhalalisha kosa (la sasa kama lipo) la Rais wa Zanzibar kula kiapo hicho kuhalalisha kinyume cha matakwa ya Muungano?
Nianze maelezo yangu kwa swali hili: Nini msingi wa Muungano? Katiba ya Muungano inapashwa kuuona na kuuchukulia vipi msingi huo?
Muungano wa Tanganyika na Zanzibar uliundwa kwa kutiwa sahihi (na waasisi wake) Mkataba wa Muungano (Articles of Union) Aprili 22, 1964 na kuridhiwa na mabunge ya nchi hizo kuwa sheria inayojulikana kama sheria ya Muungano (Acts of Union) kati ya Tanganyika na Zanzibar hapo Aprili 25, 1964, Muungano huo ukijulikana kwa jina la “Muungano wa Tanganyika na Zanzibar”. Muungano huo ulitangazwa na kuanza rasmi Aprili 26, 1964.


Dhana ya Mkataba na Sheria ya Muungano
Mkataba wa Muungano wa Tanganyika na Zanzibar ni Mkataba wa Kimataifa, ambao kwake Mataifa mawili huru yalikubali kuungana kwa mambo 11 tu, chini ya masharti kadhaa (Articles of Union) pamoja na kutoa utaratibu namna Muungano huo utakavyoongozwa. Mambo hayo 11 ya Muungano na ambayo sina sababu ya kuyaorodhesha hapa, yameelezewa vyema kwenye ibara ya nne ya mkataba huo.
Moja ya masharti ya Muungano, kwa mujibu wa ibara ya 3(b) ya mkataba huo ni kuwapo kwa makamu wawili wa Rais wa Jamhuri ya Muungano, mmoja (akiwa mkazi wa Zanzibar) atakuwa mkuu (Rais) wa Serikali ndani na kwa ajili ya Zanzibar na atakuwa pia msaidizi mkuu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano katika kutekeleza shughuli za Muungano nchini Zanzibar. Huyu atajulikana kama makamu wa Rais wa kwanza na Rais wa Zanzibar.
Ibara ya 6(a) ya mkataba huo inatamka bayana kuwa “Rais wa kwanza wa Muungano, atakuwa Mwalimu Julius K. Nyerere na ataongoza Serikali ya Muungano kwa kuzingatia matakwa ya mkataba, akisaidiwa na makamu wawili wa Rais, mawaziri na maofisa wengine atakaowateua kutoka Tanganyika na Zanzibar kwa mambo ya Muungano.
Nayo ibara 6(b) ilimtambua kwa jina, hayati Sheikh Abeid Karume, kama makamu wa kwanza wa rais na kwa mujibu wa ibara ya 3(b) ya mkataba inayoanzisha nafasi hiyo.
Mkataba wa kimataifa, kama ulivyo huu wa Muungano wa Tanganyika na Zanzibar, hauwezi kutambuliwa wala kuwa na nguvu ya kisheria kuweza kutumika mpaka uridhiwe (to ratify) na vyombo vya kutunga sheria vya nchi zilizoingia mkataba huo na kuwa sheria ya nchi (municipal law) inayotambuliwa. Hivyo ndivyo lilivyofanya Bunge la Tanganyika na Baraza la Mapinduzi Zanzibar, Aprili 25, 1964 kama nilivyoeleza mwanzo, ambapo tukaweza kupata sheria ya Muungano, namba 22, 1964.
Niharakishe kutamka mapema hapa (na hili limewahi kutamkwa pia na majaji wakuu waliopita, hayati Francis Nyalali na Barnabas Samatta kwa nyakati tofauti) kwamba makubaliano ya mkataba wa Muungano ni (mhimili wa) Katiba ya Jamhuri ya Muungano na kwamba, makubaliano hayo (Articles) yanatawala na kuwa juu ya Katiba unapotokea mgongano kuhusu Muungano.
Zaidi ni kusema kwamba, inapotokea kwamba kuna mgongano kati ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano au Katiba ya Zanzibar na Mkataba wa Muungano, matakwa ya Mkataba wa Muungano yatatawala. Hii ni kwa mantiki pia kwamba bila Mkataba wa Muungano hakuna Katiba ya Muungano, lakini si kinyume chake.
Kwa upande wa pili, Sheria ya Muungano (Acts of Union) iliyounda Muungano wa Tanganyika na Zanzibar ni hati yenye hadhi ya Kikatiba kwa sababu ndio msingi wa Muungano ambamo zinatoka taratibu na kanuni za Muungano na kupata mamlaka ya kisheria, uhalali na ridhaa ya watu kuhusu Muungano.
Kwa hiyo, Sheria ya Muungano, si sheria (ya kawaida) kama sheria zingine. Na kama ambavyo Mkataba wa Muungano hauwezi kurekebishwa baada ya kutiwa sahihi na waasisi wake miaka 47 iliyopita, ndivyo ilivyo kwa Sheria ya Muungano; na ndiyo maana haina kifungu (provision) chenye kuruhusu marekebisho.
Kifungu cha tano cha Sheria ya Muungano kinachohusu muundo na mambo yote ya Muungano, kuanzia mambo 11 ya Muungano, kuwapo kwa Bunge na Rais wa Zanzibar, uteuzi wa makamu wawili wa Rais na Katiba ya kwanza ya Muungano, ni muhimili na msingi mkuu wa Muungano, hivyo hakiwezi kamwe kufanyiwa marekebisho wala kubadilishwa (absolutely unalterable), na kwamba marekebisho yoyote yanayoweza kufanywa yatakuwa haramu na batili.
Haramu Rais wa Zanzibar kuwa Waziri
Tumeona, kwa mujibu wa Mkataba wa Muungano na Sheria ya Muungano (Hati ambazo haziwezi kufanyiwa marekebisho bila kukiuka matakwa ya Muungano) kwamba, makamu wa kwanza wa rais ndiye rais pia wa Zanzibar.
Ndiyo kusema bila ya shaka yoyote kwamba, marekebisho ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, yaliyoanzisha utaratibu wa kumpata Makamu wa Rais kwa njia ya “mgombea mwenza”, na Rais wa Zanzibar kwa njia ya kuchaguliwa na kupokonywa nafasi ya Makamu wa Rais, badala yake akapewa ujumbe wa Baraza la Mawaziri, kinyume cha matakwa ya Mkataba wa Muungano na Sheria ya Muungano, ni haramu na batili kisheria na Kikatiba.
Kwa sababu hii, Rais wa Zanzibar, Dk. Mohamed Shein, analilia na kutetea nafasi ya uwaziri yenye ubatili na kejeli ya Kikatiba kwenye Baraza la Mawaziri la Jamhuri ya Muungano.
Dk. Shein asihalalishe ubatili
Dakta Shein ameuliza: “Mbona mimi siyo wa kwanza kuapa?” Ni swali zuri, lakini ubatili hauwezi kutibiwa kwa ubatili ila kwa uhalali; lakini hapa uhalali haupo.
Ubatili juu ya ubatili, kiburi na udikteta wa chama kimoja ndivyo vimeutia Muungano wetu kwenye majaribu na tufani kubwa kwa miaka yote 47 tangu uanzishwe.
Ubatili huu juu ya muundo wa Muungano umedumu na kusalimika mabadiliko yote ya Katiba, na unaendelea kudumu katika Katiba ya 1977. Shukrani kwa udikteta wa chama, kwamba wakati makada wake (hapakuwa na msomi wa sheria hata mmoja) wakitunga Katiba hii kwa “hekima” za utanashati wa kisiasa, walipungukiwa maono juu ya mfumo wa vyama vingi mbele; sasa wanakumbuka shuka wakati kumekucha na kuishia kufanya vioja kwa suala zima la mfumo huo mpya.
Ni kwa sababu hii pia kwamba, joto la mabadiliko chini ya mfumo huu mpya wa siasa haliwezi kuisalimisha Katiba hii, kama juhudi hazitafanyika kuiokoa kwa kukubali mabadiliko muhimu ili kwenda na wakati, badala ya kuendeleza ukiritimba wa chama kimoja kwa ujanja ujanja, kana kwamba Watanzania ni mazuzu, hawana akili wala uwezo wa kufikiri.
Chimbuko la mparanganyiko
Chimbuko la mparanganyiko wa nafasi ya Rais wa Zanzibar kugeuzwa Waziri asiye na Wizara maalum ndani ya Jamhuri ya Muungano, ni ukitirimba wa Chama, kiburi na udikteta usiokubali mabadiliko na mageuzi halali.
Ni kwamba, kuingia kwa mfumo wa vyama vingi vya siasa nchini kulitoa uwezekano wa aina mbili visiwani ambao Katiba ya 1977 haikuuona wala kuutarajia. Moja ni uwezekano wa vyama viwili tofauti kutawala Zanzibar na kwa Tanzania Bara. Nguvu ya Chama cha Wananchi (CUF) visiwani, ilitoa tishio hilo kwa ukiritimba wa CCM; Wakajiuliza: “Inawezekanaje Seif Shariff Hamad (endapo CUF kitashinda Zanzibar), aruhusiwe kuwa Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano kwa mujibu wa Mkataba wa Muungano na Sheria ya Muungano?”
Kwa upande wa pili, pendekezo la kumwondolea Makamu wa Rais, urais wa Zanzibar (kama ilivyofanywa baadaye), lilizua chukizo kwa Wazanzibari na uongozi wa CCM visiwani kwa kuliona kama kitendo cha kumdhoofisha au kumvua hadhi kiongozi wao. Kwa mkanganyiko huu, suala la Makamu wa Rais liliahirishwa mara mbili bila kupatiwa ufumbuzi.
Ili kuokoa hali (na kumzuia Sharrif asipate nafasi ya Makamu wa Rais wa Muungano iwapo angeshinda) iliundwa Tume (Tume ya Jaji Mark Bomani) haraka, haraka na kutoa mapendekezo hasi na yenye utata mkubwa (kinyume cha matakwa ya Muungano), juu ya namna ya kumpata Makamu wa Rais kwa njia ya “Mgombea Mwenza” kwa mfumo wa Kimarekani.
Yalikuwa mapendekezo hasi na yenye utata kwa sababu, muundo wa Serikali mbili kwa mujibu wa Mkataba wa Muungano, umejikita kwa Rais wa Zanzibar kwa wadhifa wake kama makamu wa rais wa Muungano, akitekeleza shughuli za Muungano visiwani kwa niaba ya Rais wa Muungano.
Mara tu uhusiano huo ulipokatwa, licha ya kumuumiza Rais wa Zanzibar aliyekuwa madarakani, muundo wa Muungano ulitifuliwa, matakwa ya Muungano yakabakwa kulinda maslahi ya kichama.
Hapa, niharakishe kutamka kwamba, Makamu wa Rais wa Muungano anayepatikana nje ya utaratibu au matakwa ya Mkataba na Sheria ya Muungano, si Makamu halali wa Rais kwa mujibu wa Muungano. Wakati huo huo, mkikimkiki na fukuto la wabunge 55 (G.55) la kutaka kurejeshwa kwa Serikali ya Tanganyika lilitoa tishio kwa hatima ya Muungano; na hili la Rais wa Zanzibar kupokonywa umakamu wa Rais, nalo lilisugua kidonda kwa chumvi. Lakini CCM hakikutaka kutatua mtafaruku huo wa Kikatiba kwa kuzingatia matakwa na tafsiri sahihi ya muundo wa Muungano.
Badala yake, suala la Makamu wa Rais lilitatuliwa kinyemela kwa kumwingiza Rais wa Zanzibar kwenye Baraza la Mawaziri la Jamhuri ya Muungano, kama njia ya kumpooza maumivu ya majereha aliyopata.
Hapa maswali mengi yanazuka: Nini nafasi na wajibu wa “mjumbe” huyu katika Baraza la mawaziri? Tunajua, wajumbe wa Baraza la Mawaziri wanawajibika kwa Bunge katika umoja wao na kwa waziri mmoja mmoja kuhusu wizara yake (collective and individual responsibility), je, Rais wa Zanzibar naye anawajibika kwa Bunge, na kwa Rais wa Jamhuri ya Muungano kama walivyo mawaziri?
Katiba ya Zanzibar inayompa urais ni kwa mambo yasiyo ya Muungano visiwani. Rais wa Zanzibar anaingiaje kwenye Baraza la Mawaziri kama Rais chini ya Katiba isiyohusu Muungano? Je, anapashwa kutekeleza uamuzi wa Baraza la Mawaziri la Muungano nchini Zanzibar? Kama nani?
Ikitokea kwamba amechaguliwa Rais wa Zanzibar kutoka chama tofauti na kile kinachoongoza Serikali ya Muungano, itakuwaje? Naye atakuwa “mjumbe” wa Baraza la Mawaziri la Muungano ambalo rais na mawaziri wote ni kutoka chama tofauti? Baraza hilo litafanyaje kazi?
Jibu wanalotaka kupata wananchi hapa si kwamba “marais wengine waliomtangulia Dk. Shein walikula kiapo vivyo hivyo”, bali wanataka kujua iwapo kwa kula kiapo cha kuwa mjumbe wa Baraza la Mawaziri, ndivyo msingi wa Muungano unavyotaka? Je, ubatili unaweza kuhalalishwa na ubatili mwingine?
Viongozi wetu wanajua vyema msingi wa Muungano, lakini hawataki kutekeleza kwa usahihi na kwa moyo mweupe yanayotakiwa kwa sababu ya maslahi binafsi na ukereketwa wa kichama. Huu ndio chanzo cha tufani kwa mustakabali wa Muungano, tufani iliyodumu kwa miaka yote 47 tangu uanzishwe, huku meli ya Muungano ikiendelea kusukwasukwa kwa mawimbi yakutisha yasiyoisha. Kwa nini tunakubali kuelea hali kama hiyo, yenye kuhatarisha Muungano wetu?