Serikali za Kenya na Somalia zimekubaliana rasmi kuendelea kwa pamoja harakati zinazolenga kulitokomeza kundi la Al-Shabaab nchini somalia.

Uamuzi huu unafanyika wiki moja tangu rais wa serikali ya mpito nchini humo Shaikh Shariff Ahmed kunukuliwa akipinga kuwepo kwa wanajeshi wa Kenya nchini mwake. Lakini Waziri Mkuu Abdiweli Mohammed Ali, ameonekana kwenda kinyume na madai ya Rais Sharif, huku akisema ujumbe aliowasilisha kwa serikali ya Kenya ndio rasmi.

Kiongozi huyo alikuwa akizungumza katika kikao cha waandishi wa habari kilichoandaliwa baada ya kufanyika mkutano wa faragha kati yake na Waziri Mkuu wa Kenya, Raila Odinga.

Odinga alisema tatizo la Somalia limeathiri Kenya zaidi huku viongozi hao wawili wakitoa wito wa msaada wa dharura wa kibinadamu kwa wakazi wa Somalia katika maeneo ambayo yamekombolewa na majeshi ya Kenya.