YANGA imesema kuwa, kwa sasa imejipanga kuhakikisha inafanya usajili wa kisayansi zaidi ili kupata wachezaji wenye viwango.
Ofisa Habari wa Yanga, Luis Sendeu, ameliambia Championi Jumatano kuwa, usajili wa dirisha dogo unaotarajiwa kufungwa Novemba 30,  utafanywa zaidi na makocha wa klabu hiyo wanaoongozwa na Kosta Papic.
 Alisema safari hii makocha ndiyo watakaotoa mapendekezo kwa viongozi kuhusu wachezaji wanaowahitaji badala ya usajili kufanywa na viongozi kama ilivyokuwa awali.
“Kwa sasa katika klabu yetu, usajili utaanzia kwa benchi la ufundi ambalo litapendekeza wachezaji wa kusajiliwa kwa kamati ya usajili na ile ya mashindano.
“Baadaye kamati ya utendaji itatoa baraka za mwisho za usajili. Dirisha dogo tunataka tulitumie kwa kufanya usajili wa kisayansi zaidi kwa kulihusisha benchi la ufundi,”  alisema Sendeu.