Makanisa katika miji kadha ya Nigeria yameshambuliwa kwa mabomu.
Mripuko kwenye kanisa la Kikatoliki katika mji mkuu wa Nigeria, Abuja, umesababisha hasara kwa waumini siku ya Krismasi.
Inaarifiwa kuwa watu 25 walikufa.
Askari wa usalama wametumwa huko kuwalinda waokozi wasishambuliwe na watu.
Mripuko wa pili uliotokea kwenye kanisa, katika mji wa Jos, ulioko kati ya nchi, uliuwa askari polisi mmoja.
Kuna ripoti kuwa mripuko wa tatu umetokea mji wa Damaturu, kaskazini-mashariki mwa nchi.
Makanisa mengi, hasa katika maeneo ya kaskazini yenye Waislamu wengi, yamekuwa na tahadhari kwa sababu ya mapambano baina ya wanajeshi na watu wanaoshukiwa kuwa wafuasi wa kikundi cha kiislamu cha Boko Haram.
Ibada nyingi makanisani hazikufanywa katika eneo hilo kwa sababu ya mapambano baina ya wanajeshi na watu wanaoshukiwa kuwa wafuasi wa kikundi cha kiislamu cha Boko Haram.

Kasisi Joseph Hayet ni mshauri wa maswala ya Wakristo kwa serikali katika jimbo la Kaduna.
Aliiambia BBC kuwa usalama umezidishwa katika jimbo hilo kwa sababu ya Krismasi:
"Nimezungumza na makanisa leo asubuhi.
Walichoniambia ni kuwa watafanya ibada fupi sana, hawatazifanya ndefu; na watachukua hatua za usalama kuhakikisha kuwa hakuna anayeingia.
Taarifa moja tuliyopata ni kwamba wale wanaokusudia kuleta mtafaruku huu wanakuja na piki-piki na kurusha mabomu makanisani.
Kwa hivo makanisa yanachukua hatua kuhakikisha kuwa piki-piki hazikaribii, na hivo hawatoweza kurusha mabomu makanisani"