Waandishi wanne kati ya 15 walikuwa wamefanikiwa kupanda mlima Kilimanjaro hadi kufika kilelelni ikiwa ni sehemu ya Maadhimisho ya Miaka 50 ya Uhuru wa Tanganyika yaliyofanyika jana nchini.
Waandishi hao walifika kwenye kilele cha mlima huo wenye umbali wa mita 5,895 kutoka usawa wa bahari ni Asraji Mvungi wa ITV na Redio one, Emmanuel Almas wa TBC, Musa Juma na Mpigapicha, Emmanuel Herman wa Mwananchi.
Mwandishi Lilian Joel wa Uhuru amefika kwenye kituo cha Stella huku Charles Ndagula wa Tanzania Daima kituo cha Gilmans ambacho kiko umbali wa mita 5,650 kutoka usawa wa bahari. Daniel Mjema wa Citizen na Juma Kapipi wa Chanel Ten , Salome Kitomari wa Nipashe, Nicholaus Mmbaga wa TBC, Meneja Uhusiano wa Shirika la Hifadhi ya Taifa (Tanapa), Pascal Shelutete, Irene Mark wa Tanzania
Daima, Afisa Habari Mkuu wa Wizara ya Maliasili na Utalii, Sheila Bulu wameishia umbali wa kati ya mita 5,400 hadi 5,600.
Waandishi Rodrick Makundi na James Range waliishia kituo cha Kibo ambacho kiko umbali wa mita 4,750 kutoka usawa huo wa bahari baada ya kujisikia vibaya kutokana na mabadiliko ya hali hewa na kukosekana kwa hewa ya Oxgen ya kutosha .
Pamoja na waandishi hao, pia wahifadhi wawili Robert Mduma na Herman Mtei walifanikiwa kufika kileleni na kuweka bendera ya taifa na ya Tanapa. Waandishi hao na wahifadhi hao walifanikiwa kufika kileleni kwa msaadawa wasaidizi wa wapanda mlima Nicodemas Gobre , Mboi Seges na Masumbuko Joseph ambao muda wote walikuwa wakiwapa moyo wa kuweza kufika huko.
Waandishi hao na wasaidizi wao wakiongozwa na mzee Emanuel Minja wa miaka 81 ambaye aliishia umbali wa mita 5, 400 kutoka usawa wa bahari wapo kwenye Kituo cha Horombo kwa mapumziko kwa ajili ya kujiandaa na safari ya kuteremka hadi Geti la Marangu.
Waandishi hao walianza safari ya kupanda mlima huo Desemba 5, mwaka huu chini ya kauli mbiu ya hamasisha utalii wa ndani pinga ujangili.