Meneja Mawasiliano kwa Umma wa Sumatra, David Mziray
Mamlaka ya Usafiri wa Nchikavu na Majini nchini (Sumatra) nchini, umezifungia boti 16 na kuzinyima usajili baada ya kuonekana hazikidhi mahitaji muhimu ya usafiri huo, ikiwamo maboya, makoti ya kujiokolea pamoja na ubovu wa vyombo hivyo.
Meneja Mawasiliano kwa Umma wa Sumatra, David Mziray, alisema kupitia taarifa ya mamlaka hiyo kwa vyombo vya habari jana kuwa Oktoba na Novemba, mwaka huu pekee ilifanya ukaguzi wa vyombo vinavyotoa huduma ya usafiri katika Ziwa Victoria.
Alisema katika ukaguzi huo, boti 16 zilibainika kutokidhi mahitaji yanayotakiwa ili kuruhusiwa kuendelea kutoa huduma ya usafiri wa majini nchini. Mziray alisema vyombo hivyo vilikaguliwa katika maeneo mbalimbali ya Ziwa Victoria, yakiwamo mialo ya Kanyala, Lushamba, Kayenze na Kome.
Alisema vyombo ambavyo vimenyimwa usajili, ni vile ambavyo havikuwa na vifaa vya usalama kama makoti ya kujiokolea pamoja na ubovu wa vyombo unaohatarisha usalama.
Aliwaagiza wamiliki wa vyombo hivyo kuhakikisha vinakuwa na vifaa vyote vya usalama ndipo watakaporejeshewa usajili na leseni kuendelea na biashara ya usafirishaji abiria na mizigo. Alisema pamoja na Sumatra kupewa majukumu ya kusimamia usafiri wa nchi kavu na majini, hawataweza kufanikiwa bila ushirikiano wa vyombo vingine vya umma vyenye kujihusisha na usalama wa usafiri kama Jeshi la Polisi.
Pia uongozi wa serikali za mitaa, wamiliki na waendeshaji wa huduma za Bandari, wamiliki wa vyombo vya usafiri wa majini, watumiaji wa huduma za vyombo hivyo vya usafiri na wananchi kwa ujumla.