Na Brighton Masalu
Eti uhawara hauna talaka, ndiyo maana kuna fununu mitaani kuwa, Steven Charles Kanumba ‘The Great’ na Wema Isaac Sepetu ‘The History’, wana kila dalili ya kurudisha penzi lao la zamani.
Vyanzo cha habari na uchunguzi wa hivi karibuni wa paparazi wetu umebaini kuwa, upepo wa kimahaba wa mastaa hao, umeanza kuvuma baada ya Wema ‘kuzinguana’ na mtarajiwa wake aliyemvika pete ya uchumba, Naseeb Abdul Jumaa ‘Diamond’.
KWA NINI WARUDIANE?
Kama njiwa apelekaye habari, ndivyo mmoja kati ya shoga zake Wema alivyoleta furushi la ‘nyiuzi’ mezani na kusema, wao kama washauri wameamua kumtafutia faraja msichana mwenzao kwa kumpatanisha na Kanumba.

“Tangu habari za Diamond kutoka na Jokate Mwegelo zienee, Wema hana furaha, sisi tumemshauri arudiane na Kanumba kwa sababu ndiyo mwanaume pekee wanayeendana,” mpambe wa Wema alisema.
MIPANGO IKOJE?
Inaelezwa na mtoa habari wetu kwamba, Chatu hammezi Sungura bila kumlambalamba, hivyo harakati za kumseti Kanumba anayejifanya mgumu kimtindo, zimeanza kufanywa na akinadada wanaomsapoti ‘misezi’ Diamond aliyelia kuibiwa mumewe na Jokate.

Mbali na debe la wapambe, Wema naye anadaiwa kupewa somo na makungwi wazoefu amtegetege mpenzi wake huyo wa zamani ili cd ya penzi lao lililozimika iwakonge nyoyo, wapumzishane kimahaba.
KANUMBA ANASEMAJE?
“Sijui kama kuna jitihada za kutupatanisha zinafanywa, ila kuna siku… (akitaja jina la mtu maarufu) alinipigia simu, akaniambia habari hizo, mimi nilidhani ni utani,” Kanumba alifunguka.


Kuhusu kukutana na Wema maeneo mbalimbali na kula bata pamoja, Kanumba alisema: ”Huwa tunakutana, hasa kwenye sherehe, tunasalimiana tu, msiniharibie jamani,” kicheko cha kiana kilifuata.

WEMA ANAFAFANUA
Alipotafutwa mwanadada ambaye mbali na kujivinjari kimapenzi na Kanumba amewahi kufanya hivyo na akina kaka wengine kadhaa akiwemo mwanamuziki Charlz Baba, alisema hitaji lake kwa wakati huu ni faraja.

“Kama Kanumba anataka kurudiana na mimi atasema,” alisema Wema na kufunga ukurasa wa mahojiano na mwandishi wetu.
VIPI PENZI LA WEMA, DIAMOND?
Katika hatua nyingine, uhusiano wa kimapenzi kati ya Wema na Diamond unadaiwa kufikia kikomo hasa baada ya kuwepo kwa dai zito la Wema kuwa hataweza kumsamehe mchumba wake mpaka ampigie magoti na kukiri mbele ya umma kuwa alimsaliti, jambo ambalo Diamond amelipuuza.
                                                                             (Na GPL),