Waziri mkuu wa Zimbabwe Morgan Tsvangirai amesema uhusiano wake na mfanyabishara Locadia Tembo umefikia tamati, siku chache baada ya kutoa mahari.

Bw Tsvangirai alisema uhusiano wao "umeharibiwa na hautengenezeki" baada ya "kutekwa" na wapinzani wa kisiasa
Wawakilishi wake walitoa mahari ya maelfu ya madola na ng'ombe katika sherehe zilizofanyika Novemba 18.

Bw Tsvangirai yuko kwenye serikali ya muungano na mpinzani wake, Rais Robert Mugabe.

Katika taarifa iliyotolewa, Bw Tsvangirai, mwenye umri wa miaka, 59, alisema anatia shaka kama uhusiano wake utakuwa na "umoja thabit" na Bi Tembo mwenye umri wa miaka 39, mfanyabiashara na dada wa mbunge mmoja kutoka chama cha Bw Mugabe Zanu-PF.


"'Ndoa hii' imegubikwa na mambo mengine na kuna mkono wa kisiasa ambao sasa unaushughulisha mchakato huu," alisema kwenye taarifa hiyo.

Mke wa kwanza wa Bw Tsvangirai, Susan, alikufa kwenye ajali ya gari siku chache baada ya kuwa waziri mkuu.

'Njama nzito'


Bw Tsvangirai alikana taarifa za vyombo vya habari kuwa alikuwepo kwenye sherehe za kimila Novemba 18.

Alisema, alikuwepo ofisini mwake na kutuma ujumbe kwenye familia ya Bi Tembo "kuuweka rasmi" uhusiano huo.

Bw Tsvangirai aliongeza, "Nimekuwa mtazamaji katika uhusiano huu na mambo yanaenda haraka sana, kwenye kamera bila mimi kufahamu."

"Hii imenifanya niamini kuna njama nzito linalolikumba suala hili iliyoshusha imani yangu kwenye uhsiano huu."

Bw Tsvangirai alisema ameiarifu familia ya Bi Tembo juu ya kuvunja uhusiano huo.

"Sifa zimeharibiwa na uaminifu baina ya pande zote mbili zimepotea," alisema.

"Uhusiano huu umeharibiwa kiasi ambacho hauwezi kutengamaa na umefikia kiwango ambacho ndoa haiwezi hata kufikirika."

Shaka baina ya chama cha Bw Tsvangirai cha Movement for Democratic Change (MDC) na Zanu-PF imekuwa ikiongezeka kabla ya uchaguzi, unaotarajiwa kufanyika mwakani.
.