BBC
Mwanamume mmoja raia wa Italia alifyatua risasi katika maeneo mawili ya soko na katikati mwa mji wa Florence,na kuwaua wafanyabiashara wawili raia wa Senegal pamoja na kuwajeruhi watu wengine watatu.
Mshambuliaji huyo, Gianluca Casseri mwenye umri wa miaka 50, ni mfuasi wa kundi moja lenye kufwata siasa za mrengo wa kulia, vyombo vya habari vya nchini Italia vilisema.
Aliwaua wanaume wawili na kumjeruhi mwingine katika medani ya Dalmazia kabla ya kufyatua risasi katika medani ya San Lorenzo, na uwajeruhi wengine wawili.
Baadaye Casseri alipatikana amejiua baada ya kujipiga risasi mwenyewe, polisi wanasema.
Rais wa Italia, Giorgio Napolitano, amekataa kabisa "chuki hizi zilizojitokeza na ambazo hazina msingi" na akataka maafisa wa Italia pamoja na jamii kwa jumla "kukabiliana na watu wasiyoweza kuwastahimili wenzao na kuhakikisha kuwa kuna uwazi na mshikamano katika nchi yetu".
Meya wa mji wa Florence alielezea shambulio hilo kama wa mtu aliyekosa muelekeo.
"haya ni matendo ya muuaji mmoja - mwendawazimu na muuaji mwenye ubaguzi wa rangi," Matteo Renzi alisema, akiongeza kuwa kitendo kama hiki si sifa nzuri kwa mji huo na kimewastusha watu wengi.