Rais wa Sudan Omar al Bashir amebatilisha uamuzi wa kumtimua balozi wa Kenya nchini Sudan, baada ya kukutana na mawaziri wa Kenya.
Waziri wa mambo ya nje wa Kenya Moses Wetang'ula ambaye alikuwa pamoja na waziri wa ulinzi wa nchi hiyo Yusuf Haji, walikuwa mjini Khartoum ambako walikutana na rais Omar al-Bashir, kujaribu kutatua mzozo kuhusu amri ya mahakama ya Kenya kumkamata rais Bashir.
Jumatatu Mahakama kuu ya Kenya iliamuru serikali kuheshimu kibali kilichotolewa na mahakama ya kimataifa ya uhalifu, ICC cha kumtia nguvuni rais Bashir "kama ataingia nchini Kenya."
Waziri wa mambo ya nje wa Kenya Moses Wetang'ula, ambaye alizungumzia kuwa huenda akakata rufaa juu ya uamuzi huo wa mahakama, alisema kuwa baada ya mkutano wa Alhamisi anaamini suala hilo halitaharibu uhusiano wa nchi yake na Sudan.