Maandamano nje ya Ubalozi wa Marekani nchini Misri
 
Kumezuka ghasia zaidi nje ya ubalozi wa Marekani mjini Cairo kati ya polisi na waandamanaji wanaokashifu filamu ambayo wanasema kuwa inakejeli imani ya Kiislamu.
Runinga ya Misri ilionyesha gari likiteketezwa moto na watu wengine wakikimbia vitoza machozi.
Waandamanaji walitaka kufukuzwa kwa balozi wa Marekani nchini humo huku polisi wakiwafyatulia mabomu ya kutoa machozi waandamanaji waliokuwa wakirusha mawe.

Nchini Yemen waandamanaji wamevamia ubalozi wa Marekani wakichoma moto magari kabla ya vikosi vya ulinzi kuwadhibiti kwa kuwafukuza kutoka eneo hilo.

Maandamano zaidi pia yamefanyika katika nchi za Tunisia, Morocco, Sudan, Mauritania na Iran.

Wakati huohuo maafisa wa Marekani wanasema serikali ya nchi hiyo inachunguza ikiwa mashambulio ya jumanne kwenye ubalozi wa Marekani katika mji wa Libya wa Benghazi yalikuwa ni ya kupangwa au la .

Balozi wa Marekani nchini Libya , Christopher Stevens, aliuawa .

Maafisa wa Marekani wameelezea mashambulio hayo kama yenye utata na yenye kupangwa kitaalamu na kuna tetesi kwamba makundi ya jihad huenda yalihusika .

Awali ilifikiriwa kuwa mashambulio hayo yalikuwa na uhusiano na maandamano ya kupinga filamu iliyokuwa inamkejeli Mtume Mohammed.

Takriban waandamanaji mia mbili wamekusanyika karibu na ubalozi wa Marekani mjini Cairo Misri kwa usiku wa pili kuelezea hasira yao juu ya filamu hiyo .
Awali waandamanaji walirusha mawe kwenye ubalozi huo na vikosi vya usalama vikafyatua mabomu ya kutoa machozi kuwa tawanya.

Watu wenye silaha waliokuwa na maguruneti walichomo moto jengo la ubalozi na walioshuhudia wanasema watu hao walizingira eneo hilo.

Rais Obama amelaani vikali shambulio hilo na ameahidi kushirikiana na serikali ya Libya kuwafikisha mbele ya sheria wahusika