Mwenyekiti wa Jumuiya ya Madaktari walioathirika na mgomo Dr. Paul Swakala (katikati) akizungumza na waandishi wa habari jijini Dar es Salaam.
Na. Datus Boniface
Wanaodaiwa kuwa ni Madaktari wanaofanyakazi chini ya usimamizi wa madakatari bingwa (Intern Doctors), wamemwangukia Rais Jakaya Kikwete huku wakimwomba radhi kwa ushiriki wao katika mgomo wa madaktari uliosababisha maafa kwa baadhi ya wagonjwa.
Kwa upande mwingine wamekijua juu Chama Cha Madaktari Tanzania (MAT) kuwa kimewasaliti katika kutatua matatizo yao kwa sasa.
Hata hivyo, wameomba radhi kwa Wananchi walioathirika na mgomo huo kwa usumbufu uliyosababishwa na mgomo huo.
Hadi sasa Madaktari 364, wako mtaani baada ya kusimamishwa kazi kutokana na kushiriki katika mgomo ambao umeisha hivi karibuni, baada ya kushawishiwa na wenzao wakiwemo viongozi wa MAT.
Akitoa tamko kwa waandishi wa habari jijini Dar es Salaam, Mwenyekiti wa Jumuiya ya Madaktari hao, Paul Swakala alisema “Tulikaa na MAT kuzun gumza juu ya kutusaidia kutatua kero zetu lakini wameshindwa kutusikiliza na baadala yake tumeamua kufika hapa na kutoa kilio chetu”
Kutokana na kusalitiwa huko, alitoa onyo kwa Madaktari wengine kuwa wanaweza kupima kama wataendelea kujiunga na MAT au la.
Alienda mbali zaidi na kusema, hawako tayari tena kushiriki kwa namna yoyote katika migomo inayoweka rehani maisha ya Watanzania.
Alisema, kwa hakika wanajutia kosa lao la kushiriki mgomo na wako tayari kurejea kazini ili kuendelea na kazi ya kuwahudumia Wananchi kwa moyo mweupe.