Mshambuliaji wa kujitoa mhanga ameuawa katika shambulizi la bomu ambalo limetokea mjini Mogadishu na kuwaua watu 14.

Shambulizi hilo limetokea karibu na mkahawa mmoja mjini Mogadishu. Walioshuhudia tukio hilo wamesema kuwa watu kadhaa wamejeruhiwa.
Hadi sasa hakuna kundi lolote limeelezea kufanya shambulizi hilo.

Shambulizi la leo linatokea wakati majeshi ya Somalia yanakaribia kuuzingira mji wa Kismayo ambayo ni ngome kubwa na ya mwisho ya Al Shabaab.

Shirika la umoja wa mataifa la kuwahudumia wakimbizi UNHCR limeelezea kuongezeka kwa idadi ya watu wanaotoroka mji wa Kismayo ambao sasa wanafikia zaidi ya elfu moja kila siku.

'Mlipuko wa pili'


Mwandishi wa BBC mjini Mogadishu, Ibrahim Aden, ameelezea kuona zaidi ya miili sita katika mkahawa huo ambao uko mkabala na ukumbi wa michezo ya kuigiza baada ya shambulizi.
Ameongeza kuwa eneo hilo ni maarufu kwa wafanyakazi wa umma pamoja na waandishi wa habari.Waandishi wawili wanasemekana kuwa miongini mwa wale waliouawa.

Baadhi ya waliojeruhiwa walipelekwa hospitalini wakiwa na majereha mabaya.

Taarifa ambazo hazijathibitishwa zinasema kuwa mlipuko wa pili vile vile ulitokea karibu na mkahawa wakati watu walipokusanyika kushuhudia kilichotokea.