Kamanda wa polisi mkoa wa Singida ACP Linus Sinzumwa akitoa taarifa ya wahamiaji haramu kutoka Ethiopia kwa waandishi wa habari (hawapo kwenye picha).
 
Picha na Nathaniel Limu.
Jeshi la polisi mkoa wa Singida linawashikilia raia watano wa nchini Ethiopia kwa tuhuma ya kuingia na kuishi katika Jamhuri ya Muungano wa Tanzania bila ya kuwa na kibali.
Akizungumza na waandishi wa habari ofisini kwake Kamanda wa polisi mkoa wa Singida ACP Linus Sinzumwa, amesema wahamiaji hao haramu, wamekamatwa septemba 18 mwaka huu saa kumi jioni wakiwa ndani ya nyumba ya kulala wageni ya Singida Modern iliyopo Kibaoini.
Sinzumwa amesema kuwa raia hao ambao bado haijajulikana wameingilia wapi na walikuwa wakielekea nchi gani, wamekamatwa baada ya raia wema kutoa taarifa polisi.
Kamanda Sinzumwa amesema kuwa hivi sasa vijana hao kutoka Ethiopia, wanaendelea kuhojiwa na maafisa wa uhamiaji na mara mahojiano hayo yatakapomalizika, watuhumiwa watafikishwa mahakamani kujibu tuhuma inayowakabili.