Hailemariam Desalegn
Waziri mkuu mpya wa Ethiopia Hailemariam Desalegn, ameapishwa kuchukua wadhifa wa hayati Meles Zenawi aliyeitawala nchi hiyo kwa miaka 21.

Mwingine aliyeapishwa ni naibu wake Demeke Mekonen, ambaye alikuwa anashikilia wadhifa wa waziri wa elimu.
Bwana Hailemariam Desalegn, amenukuliwa na shirika la habari la AFP akisema kuwa ana furaha kuchukua wadhifa huo na yuko tayari kufanya majukumu yake kwa kujitolea.

Hailemariam aliungwa mkono bila pingamizi na bunge la waakilishi ambalo lina wanachama wengi wa muungano tawala kuchukua wadhifa huo

Sherehe ya kumuapisha waziri mkuu huyo iliendeshwa na rais wa mahakama ya juu zaidi nchini humo, Tegene Getaneh na kuonyeshwa moja kwa moja kupitia televisheni ya taifa.

Hayati Zenawi alifariki mwezi jana mjini Brussels baada ya kuugua kwa muda mrefu.