Na Shakoor Jongo
Wadau na mashabiki wa mastaa wawili nchini, Wema Sepetu wa Bongo Movie na Nasibu Abdul ‘Diamond’ wa muziki wa kizazi kipya, wamebariki ndoa ya wapenzi hao kwa kusema kuwa ni watu wanaoendana na kutegemeana kwa kiasi kikubwa.

Mwanzoni mwa wiki hii, Wema na Diamond walitupia katika kurasa zao za mitandao ya kijamii picha zao, ambazo zinaonekana zilipigwa eneo moja kwa simu moja na hivyo kuwapa wakati mzuri mashabiki wao ambao walionekana kupendezwa na uhusiano wao na kupendekeza waoane.
“Hii ndiyo couple bomba zaidi ya wasanii Bongo, kwa nini msioane? Mnapendeza sana jamani, ebu Diamond Platnumz achana na Penny bwana, huendani naye kwanza kuna mambo ya dini na nini…,” aliandika shabiki mmoja.

Mwingine aliandika: “Nadhani Penny angejiweka tu pembeni awaache hawa wawili, ni mastaa kwa fani zao, yeye angeendelea tu na kazi yake ya utangazaji. Kwanza kwake ni maumivu tu kuwa na msanii ambaye ana shughuli nyingi za kisanii, bora wale wenyewe wanajuana.”
Ingawa kwa muda mrefu Diamond amekuwa akikanusha kurudiana na Wema, hivi karibuni picha zao zilivuja katika mitandao ya kijamii wakiwa China wakila bata na alipoulizwa, ‘alizuga’ eti walikuwa wakitengeneza filamu.
Hata hivyo, uchunguzi wa gazeti hili umebaini kuwa, wadau wengi wanaamini Wema na Diamond wanapendana kwa dhati hivyo wakapendekeza wafunge ndoa na kuyaacha maisha mengine yaendelee kuwepo kuliko kuachana kisha kurudiana mara kwa mara.