Wapiganaji nchini Libya wameteka ofisi na majengo ya wizara za serikali mjini Tripoli.
Hii ni kwa mujibu wa taarifa ya serikali ya nchi hiyo.Watu waliokuwa wamejihami waliwazuia wafanyakazi kuingia katika ofisi za wizara hizo.
Mnamo siku ya Jumapili, wapiganaji hao waliteka makao ya ubalozi wa Marekani.
Libya imekumbwa na vurugu tangu kung'olewa mamlakani kwa hayati kanali Muammar Gaddafi aliyepinduliwa na wanajeshi wa Nato wakisaidiwa na wapiganaji wa kiisilamu mwaka 2011.
Wapiganaji hao wamekuwa wakipigana miongoni mwao wenyewe wakitaka mamlaka.
Maafisa wakuu wa serikali na wabunge walihamia katika mji wa Tobruk, Mashariki mwa nchi hiyo mwezi jana.
Marekani na mataifa mengine yalilazimika kuwaondoa wafanyakazi wao kutoka nchini humo mwezi Julai huku mapigano yakichacha mjini Tripoli.
Benki kuu ya Libya pamoja na kampuni ya mafuta inayomilikiwa na serikali ziko mjini humo.
Waziri mkuu Abdullah al-Thinni na baraza lake la mawaziri, walijiuzulu wiki jana ili bunge liweze kuteua serikali mpya.
Uchaguzi huo ulikuwa wa pili tangu kanali Gaddafi kuuawa katika mapinduzi ya mwaka 2011. Matumaini ya uchaguzi huu kurejesha uthabiti nchini Libya ni hafifu mno.