Stori: Mwandishi Wetu
Ni shida! Jeshi la Polisi Kikosi cha Usalama Barabarani Tanzania, chini ya Kamanda Mohammed Mpinga, limekuwa mstari wa mbele katika kusimamia maadili ya askari wake na kuwa mfano wa kuigwa lakini kuna baadhi wanalichafua, Ijumaa limenyetishiwa kamchezo kamili.HABARI KAMILI
Habari kamili ikufikie kwamba nyuma ya picha ya askari wawili, mwanamke na mwanaume wa usalama barabarani (matrafiki) wanaodaiwa kuacha kazi ya kuongoza magari na kwenda kufanya uchafu kichakani kuna utata mkubwa.
PICHA INASEMA

Picha hiyo inamuonesha trafiki mwanamke akiwa amepakatwa mapajani na trafiki mwanaume aliyekalia kitu kwa chini ili kupata balansi ya kumbeba mwenzake huku wawili hao ‘wakifanya yao’ wakiwa na sare za kazi.

TUJIUNGE NA VYANZO

Baada ya picha hiyo kusambaa kwa kasi ya moto wa kifuu kwenye mitandao mbalimbali ya kijamii usiku wa kuamkia Jumatano wiki hii na kugeuka habari ya mjini, watu walikuwa na maoni tofauti huku baadhi wakipiga simu kwenye chumba chetu cha habari wakitaka kujua ukweli juu ya uwepo wa tukio hilo.

SIMU YA KWANZA

Simu ya kwanza iliyopigwa ilidai kwamba matrafiki hao ni maarufu katika Barabara ya Bagamoyo ambapo mara nyingi huongoza magari maeneo ya Tegeta jijini Dar.“Huyo mwanaume ni jamaa mmoja mpole sana anajulikana Tegeta na ana gari aina ya Baloon (Toyota).

“Huyo mwanamke, kwanza ni mke wa mtu lakini yupo bomba (mzuri) kinoma. Hata madereva daladala wanamjua maana amejaliwa, akitembea lazima atingishe,” kilidai chanzo hicho na kuongeza:

“Hapo ni maeneo ya Tegeta kwa sababu ukiangalia vizuri kwenye picha hiyo utaona nguzo ya umeme mkubwa wa Zanzibar.”

WHATSAPP

Wakati tukio likiwa ‘hot’, picha hiyo ilitumwa kwenye chumba chetu cha habari kwa WhatsApp huku ikiwa na maelezo kwamba tukio hilo lilijiri hivi karibuni mkoani Dodoma bila kufafanua maeneo gani kwa kuwa Dodoma ni kubwa. 

NI KANDA YA ZIWA?

Chanzo kingine kilichozungumza na gazeti hili kilidai kwamba tukio hilo siyo la Dar wala Dodoma ni maeneo ya Kanda ya Ziwa.
“Hilo tukio ni la Kanda ya Ziwa. Itakuwa ni kwenye moja ya Mikoa ya Kanda ya Ziwa (kati ya Mwanza, Mara, Kagera, Shinyanga, Simiyu na Geita),” kilidai chanzo hicho.

IMETENGENEZWA?

Baadhi ya wadau wa jeshi hilo walidai kwamba kuna uwezekano picha hiyo ni ya kutengeneza (photo shop) kwa kuwa haikujulikana aliyeipiga na kwamba iliwezekanaje kuwapiga ili hali wakijua ni kinyume na maadili.

“Unajua kinachonifanya nihisi kama imetengenezwa ni namna walivyojiachia. Kwa vyovyote kuna kitu cha ziada kimefanyika kwenye hiyo picha,” alisema mmoja wa wachangiaji mtandaoni.
MTAALAM: HAIJATENGENEZWA

Ili kuondoa utata huo wa kutengenezwa au kutokutengenezwa, gazeti hili lilimwonesha picha hiyo, mtaalam wetu wa kompyuta (IT), Nicolaus Trac ambaye alithibitisha kuwa siyo ya kutengenezwa.
“Ni vigumu kuwa ni ya kutengenezwa kwa sababu kuu tatu.
“Moja, mandhari ni moja, ingekuwa ya kutengeneza kila mmoja angeonekana tofauti lakini mazingira yanaonesha imepigwa eneo moja.

“Pili, angalia mikono yao ilivyovaana au kuingiliana. Sidhani kama kuna mtaalam angeweza kuweka mikunjo hiyo ya mikono na vidole bila kukosea sehemu.

“Tatu, angalia huyo mwanamke alivyomkalia mwanaume, inaonesha kabisa kumkalia kwake kumesababisha mkunjo katika suruali kwenye paja la mguu wa kulia,” alifafanua Nicolaus.

PETE YAIBUA MAMBO

Mbali na kukemea tabia hiyo na ukosefu wa maadili hasa kwa mtumishi wa serikali, wapo baadhi ya watu mitandaoni walikuwa wakimshambulia trafiki mwanamke kwani picha ilimuonesha akiwa na pete ya ndoa kidoleni.

“Mimi sijui kama huyo trafiki ni mumewe lakini namuona ana pete ya ndoa maana yake kuna harufu ya mchepuko. “Lakini hata kama ni mumewe, kwa nini wafanye mambo ya chumbani hadharani tena na sare za kazi? Kama walikuwa wamezidiwa sana si wangeenda nyumbani?” Alihoji mwanamke mmoja aliyetumiwa picha hiyo kwenye WhatsApp.
KAMANDA MPINGA ANASEMAJE?

Gazeti hili lilimfowadia Kamanda Mpinga picha hiyo kwa njia ya WhatsApp ambapo alikiri kuwa nayo na kwamba  wanaifanyia kazi kabla ya kuchukua hatua kali kwa wahusika.
Katika mahojiano ya Kamanda Mpinga na Global TV Online hivi karibuni, kamanda huyo alisisitiza kwamba kikosi chake kinaongoza kwa maadili na kwamba inapotokea tukio kama hilo hutolewa adhabu kali.