Stori: Hamida Hassan na Imelda Mtema
Mastaa wa filamu Bongo, Blandina Chagula ‘Johari’ na Chuchu Hans  ambao wamekuwa katika bifu kwa muda mrefu kutokana na uhusiano wa kimapenzi na Vincent Kigosi ‘Ray’, hivi karibuni nusu wazichape kwa mara nyingine baada ya kurushiana matusi mazito ya nguoni.Tukio  hilo lilijiri juzikati katika hoteli moja iliyopo Sinza jijini Dar.
Chanzo cha uhakika kilichokuwa eneo la tukio kinavujisha kwamba, Ray alifika katika hoteli hiyo akiwa katika teksi na aliandamana na Chuchu.

Inadaiwa Ray alifika hotelini hapo kwa ajili ya kuonana na mkurugenzi mwenza wa kampuni yao ya RJ, Johari, ambaye kwa wakati huo alikuwa akisimamia kambi ya projekti yao mpya.
Baada ya Ray kushuka kwenye teksi na kuingia ndani ya hoteli hiyo huku Chuchu naye akishuka kwenye na kusimama nje akimwangalia mwandani wake anavyomsogelea Johari ambaye siku za nyuma alikuwa ndiye mwandani wake.
Kitendo cha Chuchu kutokeza kuonesha alikuwa ameandamana na mkali huyo wa filamu kilimchukiza Johari ambaye kwa sauti iliyosikika vyema, alimuuliza Ray kwa nini alikwenda akiwa ameongozana na ‘malaya’ wake.“Matusi yale yalimkera sana Chuchu, naye aliamua kumrudishia hali iliyosababisha kutokea kwa tafrani kubwa kwani watu walianza kujazana na kuwazuia wasichapane,” kilisema chanzo chetu.
Baada ya habari hii kutua mezani, mapaparazi wetu waliingia kazini ili kuujua ukweli, mtu wa kwanza kuzungumza naye ni Johari ambaye siku za nyuma aliwahi kuzichapa na mpinzani wake huyo wakati akilitetea penzi lake lililokuwa likiyumba.
Johari alikiri kutokea kwa tukio hilo na kudai kuwa mwigizaji huyo alikwenda kambini kwake kufanya fujo ambazo hata hivyo alishindwa kufafanua.
Kwa upande wake, Chuchu alipoulizwa alisema: “Nimemvumilia sana Johari, amekuwa akinitukana kila kukicha nanyamaza, sasa nimechoka na kibaya zaidi siku hiyo alinitukania mama yangu, nimekuwa nikimvumilia kwa sababu alikuwa akinitukana mimi, sasa kumuingiza mama kwenye ugomvi wetu siwezi kumvumilia kamwe,” alisema Chuchu.