Timu ya Vijimambo inamasikitiko makubwa ya habari ya upotoshaji iliyoandikwa na gazeti la Jamhuri lililobeba kichwa cha habari "AUNTY EZEKIEL ATANUA NA WAZIRI NYALANDU MAREKANI" yakiwemo magazeti mengine yaliyodandia kuandika habari hii bila kujua ukweli upo wapi. Timu ya Vijimambo ikiwemo kamati ya maandalizi imechukizwa sana kwa Gazeti hili kuandika habari ya kizushi na inayojeruhi hisia ya familia ya Mhe. Waziri  Lazaro Nyalandu. 

Habari hii ni uongo ulioandikwa kichochezi na mwandishi anayeitwa Alfred Lucas. Timu ya Vijimambo haikufurahishwa na uongo huu pamoja na VIJIMAMBO BLOG kuwa ndio wahusika wakuu, mwandishi alitakiwa kutupigia simu ili aweze kupata habari ya upande wa pili.


Masanja Mkandamizaji na Shilole walipokuja mwaka 2013 kwenye sherehe ya miaka 3 ya Vijimambo iliyobeba ujumbe wa Tamasha la Utamaduni wa Kiswahili



Kwa kumsikiiza Aunty Ezekiel mwenyewe anasemaje kuhusu habari hii kama anavyoripoti Mubelwa Bandio wa Kwanza Production bofya play





Waziri wa Maliasili na Utalii Mhe. Lazaro Nyalandu katika picha ya pamoja na Balozi wa Tanzania nchini Marekani Mhe Liberata Mulamula, Maafisa na wafanyakazi wa Ubalozi wakiwemo wadau wa Kimarekani wanaotangaza Utalii wa Tanzania nchini Marekani. Mhe. Lazaro Nyalandu alikutana na wadau wa Utalii siku ya Ijumaa Sept 12, 2014 kwenye Ubalozi wa Tanzania nchini Marekani na wadau walipomueleza Mhe. Waziri dukuduku lao na changamoto wanazokabiliana nazo wanapowapeleka Watalii Tanzania.


Katika gazeti hilo pia limeandika "Aunty Ezekiel amekaa Marekani siku 14"  Ndugu mwandishi Aunty Ezekiel amekaa Marekani siku 10 tu amekuja Sept 13, 2014 na ameondoka Sept 24, 2014 na Aunty Ezekiel hakuja kupumzika huku na Waziri kama ulivyopotosha na uandishi wako wa uchochezi, uliojaa chuki na husda kama nilivyosema hapo awali kwamba Aunty Ezekiel ameingia Marekani siku ya Jumamosi Sept 13 na Mhe. Waziri Lazaro Nayalndu ameingia Marekani siku ya Ijumaa Sept 12, 2014. Aunty Ezekiel na msanii mwingine wa Bongo Flava Kassim Mganga safari zao zimeratibiwa na Kamati nzima ya Vijimambo kwa ushirikiano wa Ubalozi wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania nchini Marekani na Jumuiya ya Watanzania DMV huku wakiwezeshwa na wadhamini mbalimbali waliojitokeza kudhamini tamasha hilo la Utalii.

Wenyeji wa wasanii hawa walikua timu ya Vijimambo pamoja na kamati yake. Lengo la wasanii hawa kama walivyokuja wasanii Masanja Mkandamizaji na Shilole ni kuonyesha utamaduni wetu na Utalii kupitia soko la wasanii wa Tanzania ikiwemo kuwatangaza wasani wetu kimataifa.


Waziri Lazaro Nyalandu akizindua kampuni ya Utalii Sept 16, 2014 jimbo la California kampuni inayomilikiwa na Balozi wa heshima Ahmed Issa.



Ndugu mwandishi Aunty Ezekiel na Waziri wameonana mara moja tu usiku wa Sept 13, 2014 kwenye kilele cha sherehe ya Utalii na baada ya hapo hawakuwahi kuonana tena na baada ya sherehe ya Utalii Jumatatu Mhe. Waziri Nyalandu alisafiri kuelekea California kuzindua kampuni ya Utalii ya Tanzania Safari and Tourism inayomilikiwa na Balozi wa Heshima Ahmed Issa na hakuwahi kurudi tena Washington, DC mpaka siku aliyoondoka.


Msanii Shilole akimsalimia Rais mstaafu Mhe. Ali Hassan Mwnyi alipokuja mwaka 2013 kwenye Tamasha la utamaduni la Kiswahili nchini Marekani.



Ndugu mwandishi sababu iliyomleta Mhe. Waziri nchini Marekani ni kutokana na ujumbe wa Utalii na kukemea ujangili na Mhe.. Lazoro Nyalandu ndiye aliyekuwa mgeni rasmi kama ilivyokua kwa Rais Mstaafu Ali Hassan Mwinyi alipokua mgeni rasmi kwenye tamasha la Utamaduni la Kiswahili.


Naibu Waziri wa Sayansi na Teknologia Mhe. January Makamba na mkewe wakiwasili uwanja wa ndege wa kimataifa wa Dulles huku wakipokelewa na Afisa Mindi Kusiga wakati huo akiwa Ubalozi wa Tanzania nchini Marekani, kushoto ni Mwenyekiti kamati ya Vijimambo Bw. Baraka Daudi.Mhe. Janauary Makamba alikua mgeni rasmi wa sherehe ya Uhuru miaka 51.


 Tunaiomba Serikali kuyachukulia hatua zinazositahili magazeti kama haya yanayoweza kujeruhi hisia ya mtu na habari ya uongo kama hii ni sumu kubwa kwenye mahusiano na upendo kwa familia na siku zote habari ya uongo hua na nguvu kuliko ukweli.

Mwisho timu ya Vijimambo na kamati ya maandalizi tunaomba radhi kwa Mhe. Waziri Lazaro Nyalandu kwa usumbufu na maumivu ya gazeti la Jamhuri na magazeti mengine yaliyodandia habari yalivyosababisha kwako na familia yako. Siku zote tutakua mstari wa mbele kufanyakazi na wewe popote na wakati wowote.


Aunty Ezekiel akitia saini kitabu cha wageni Ubalozi wa Tanzania Umoja wa Mataifa New York, kulia ni Balozi Tuvako Manongi Balozi wa Tanzania Umoja wa Mataifa.