Zanzibar: 
Katibu Mkuu wa CUF, Maalim Seif Sharif Hamad amesema chama chake kitazunguka nchi nzima kupiga kampeni ili wananchi waikatae Katiba Inayopendekezwa.
Alisema watafanya hivyo kwa kuwa Katiba iliyopendekezwa imepoteza uhalali kwa vile theluthi mbili (ya wajumbe wa Zanzibar) inayodaiwa kupatikana haiwiani na takwimu za wabunge waliokuwamo ndani na nje ya Bunge na wale waliopiga kura ya hapana na kuwataka wananchi kuikataa wakati ukifika.
Maalim Seif ambaye pia ni Makamu wa Kwanza Zanzibar, alisema hayo jana akihutubia mkutano wa hadhara wa kwanza tangu Katiba hiyo inayopendekezwa kukabidhiwa kwa Rais Jakaya Kikwete na Rais wa Zanzibar, Dk Ali Mohamed Shein ikipendekeza mfumo wa Muungano wa serikali mbili badala ya tatu KAMAilivyokuwa imependekezwa na rasimu iliyotokana na maoni ya wananchi yaliyokusanywa na iliyokuwa Tume ya Marekebisho ya Katiba.
Alisema kwa kutumia uwezo wake wa kisiasa na mbinu nyingine, atahakikisha anawashawishi wananchi kupiga kura ya hapana ili kuipinga kwa vile haina masilahi kwa Zanzibar.
“Imelenga kupunguza mamlaka kamili ya Zanzibar ya kikatiba na nawashangaa wabunge wa CCM walioacha kujadili Rasimu ya Jaji Warioba na kutunga rasimu yao na kuipitisha wao wenyewe na baadaye kucheza ngoma wakati rasimu hiyo imemeza mamlaka ya Zanzibar,” alisema.
Hata hivyo, alisema hafikirii kujiuzulu wadhifa wake wa Makamu wa Rais licha ya kutoridhishwa na mchakato wa huo.
“Nitaendelea kushika wadhifa wangu wa Makamu wa Rais, tutabanana humuhumu, nitatetea mamlaka kamili ya Zanzibar nikiwa ndani ya Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar na kamwe sitajiuzulu, hadi uchaguzi mkuu wa mwakani, tutakapoishika wenyewe Serikali ya Umoja wa Kitaifa” alisema Maalim Seif.