TAHARUKI imezuka katika Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Jomo Kenyatta (JKIA), Nairobi nchini Kenya, jana asubuhi baada ya abiria aliyekuwa mgonjwa kufariki dunia muda mfupi alipowasili uwanjani hapo.
Abiria huyo mwanamke alikuwa akitokea Juba, Sudan Kusini lakini kukawepo tetesi kuwa huenda amefariki kwa ugonjwa wa Ebola.
Vipimo vya madaktari vimeonesha kuwa mgonjwa huyo hakufa kwa Homa ya Ebola. Katibu wa Afya wa Baraza la Mawaziri nchini Kenya, James Macharia amethibitisha kuwa mgonjwa huyo hakuwa na Homa ya Ebola.

Mashuhuda wa tukio hilo wamesema kuwa waliwaona maofisa wa afya wakielekea katika Kliniki ya Port ambapo mgonjwa huyo alikimbizwa kabla ya mauti kumfika.
Viwanja vya ndege ni baadhi ya maeneo yaliyo katika uangalizi kutokana na ugonjwa hatari wa Ebola ambao mpaka sasa umeua watu zaidi ya 4,000 kwenye ukanda wa magharibi mwa Afrika. 
Shirika la Ndege la Kenya Airways lilisitisha safari zake katika ukanda wa magharibi mwa Afrika kwa kuogopa maambukizi ya ugonjwa huo.