aweso
Ndugu Jumaa Aweso.
Na Mohammed Hammie, Pangani, Tanga
Mtoto wa mama ntilie mwenye uzao halisi kutoka wilayani Pangani mkoani Tanga, Ndugu Jumaa Aweso (pichani) ameibuka na ushindi wa kishindo katika uchaguzi wa ndani wa chama cha mapinduzi CCM.
Akitangaza matokeo ya uchaguzi huo katibu wa CCM wilayani Pangani Bi Zaina Mlawa amesema kuwa, katika uchaguzi huo uliowashirikisha wagombea wapatao kumi na moja, Ndugu Aweso amekuwa wa kwanza miongoni mwa wagombea hao.
Uchaguzi huo uliokuwa na ushindani wa aina yake kutokana na kuwepo kwa aliyekuwa Mbunge wa jimbo hilo Ndugu Salehe Pamba, uliwashirikisha wapiga kura wapatao 10376 wa chama cha mapunduzi.
Awali wakati akitangaza matokeo ya uchaguzi huo, Bi Zania aliwataja wagombea hao kwa idadi ya kura walizopata na kusema kuwa "Ndugu Wahi Ibrahim amepata kura 87, ndugu Rosemary Luanda amepata kura 89, ndugu Elizabeth Alatanga amepataa kura 158, Halima Kimbau amepata kura 222, Ndugu Mohammed Rished amepata kura 442, Ndugu Ayubu Mswahili amepata kura 565"
Bi Zania ameongeza kwa kusema kuwa "Ndugu Omary Mwidadi amepata kura 587, ndugu Omary Chambega amepata kura 720, ndugu Salehe Pamba amepata kura 1567, ndugu Abdurahmani magati amepata 1956, na ndugu Jumaa Aweso 3983"
Ushindi huo kwa ndugu Jumaa Aweso unampa nafasi ya kuwa mgombea wa kwanza katika kuipeperusha bendera ya chama cha mapinduzi CCM wilayani Pangani endapo kamati kuu ya maamuzi itaridhia.
Mpaka sasa katika jimbo la Pangani kumepatikana wagombea wawili ambao wanaonekana kupendwa sana na wanancho ambao ni Amina Mwidau wa CUF pamoja na JUmaa Aweso wa CCM ambapo kwa mujibu wa wachambuzi wa masuala ya siasa, endapo watakutana katika nafasi ya ubunge upinzani utakuwa wa aina yake.