SIASA katika ubora wake! Nyota wa filamu nchini, Jacqueline Walper Massawe ‘Wolper’ amemchana staa mwenzake, Chuchu Hans kufuatia kutofautiana kiitikadi kisiasa kati ya chama tawala (CCM) na Ukawa.
Nyota wa filamu nchini, Jacqueline Walper Massawe ‘Wolper’.
Awali, Chuchu Hans alitangaza kuhamia Ukawa (Umoja wa Katiba ya Wananchi) na kushiriki kikamilifu kwenye uzinduzi wa kampeni zao uliofanyika katika Viwanja vya Jangwani, Dar wiki iliyopita.
Chuchu Hans.
Lakini ghafla, Chuchu alionekana akiwa amevaa sare za Chama Cha Mapinduzi (CCM) na kutangaza kwamba ameamua kurudi nyumbani, kitendo kilichoonekana kumkera mno Wolper, ambaye amejipambanua kuwa ni mfuasi namba moja wa mgombea urais wa Chadema, Edward Lowassa.

“Sijui huu uzalendo wa Tanzania utakuja lini, yaani wewe juzi tuwe wote na sare uvae, leo umetusaliti kisa vijisenti sasa aliyekwambia Ukawa tunapewa hela ukaja na mbwembwe zote nani? Sikuwa na lengo la kukuweka hapa ila nataka niseme kitu kimoja, jamani hamna kitu kibaya kama unafiki, tamaa na njaa, hii ni nchi yetu sasa tukihongwa wote ili tuwe chama kimoja ukombozi utakuwa wapi,” ilisomeka sehemu ya waraka ambao msanii huyo aliuweka katika mtandao wake wa Instagram.

Gazeti hili lilimtafuta muigizaji huyo ambaye ni mpenzi wa Vincent Kigosi ‘Ray’ na alipotakiwa kuzungumzia jambo hilo, alifunguka:
“Sikutaka kujibu, lakini nimwambie Wolper ingawa mimi nimewahi kuzaa, lakini yeye ni dada yangu, kanizidi umri, kwenye siasa kila mtu ana haki ya kupenda kule anakotaka mwenyewe. Ni kweli nilienda Ukawa, lakini baadaye nikagundua hawana ‘ishu’ nimerudi zangu CCM.”