BAADA ya Rais John Magufuli, kuagiza fedha zilizochangwa kwa ajili ya kugharamia hafla ya wabunge zipelekwe katika Hospitali ya Taifa Muhimbili (MNH) kwa ajili ya kununulia vitanda vya wagonjwa, leo Katibu Mkuu Kiongozi, Balozi Ombeni Sefue anatarajia kufanya ziara katika hospitali hiyo.
Kwa mujibu wa Kaimu Mkurugenzi wa Mawasiliano Ikulu, Gerson Msigwa, lengo la ziara hiyo ni kukagua utekelezaji wa maelekezo ya Rais Magufuli aliyoyatoa hivi karibuni ya kutaka fedha zilizochangwa kwa ajili ya hafla ya wabunge, zitumike kununulia vitanda vya wagonjwa katika hospitali hiyo.

Mara baada ya kuhutubia Bunge la 11, alipohudhuria hafla ya kuanza kazi rasmi kwa Bunge hilo, Rais Magufuli, aliagiza kati ya kiasi cha Sh milioni 225 kilichochangwa kwa ajili ya hafla hiyo, Sh milioni 24 ndio zitumike kugharamia hafla hiyo na nyingine zote zikanunulie vitanda vya wagonjwa.
Dk Magufuli alipata taarifa za kuwepo kwa michango hiyo ya fedha na kutoa maelekezo kuwa zitumike kwa kiasi kidogo kwa ajili ya hafla hiyo na sehemu kubwa zipelekwe MNH ili zikatumike kununulia vitanda na hivyo kupunguza tatizo la wagonjwa wanaolala chini kutokana na uhaba wa vitanda unaikabili hospitali hiyo.
“Nilipoambiwa kwamba zimechangwa Sh milioni 225 kwa ajili ya sherehe, nikasema fedha hizo zipelekwe Muhimbili zikasaidie kununua vitanda,” alisema na kuongeza: “Kwa kufanya hivyo tutakuwa tumejinyima sisi wenyewe, lakini tutakua tumewanufaisha wenzetu ambao wana matatizo makubwa yanayoweza kutatuliwa kwa fedha hizo.”
Awali, katika hafla hiyo, wakati akitoa taarifa ya michango hiyo, Ofisa wa Spika wa Bunge, Said Yakubu alisema jumla ya michango iliyopatikana ni Sh milioni 225 na kwamba fedha zilizotumika katika hafla hiyo ni Sh milioni 24 tu baada ya kuzingatia maagiza ya Rais Magufuli.
Pamoja na agizo hilo, siku nne, baada ya kuingia ofisini Ikulu, Dk Magufuli alifanya ziara ya kushitukiza Muhimbili na kulazimika kuivunja Bodi ya Wakurugenzi ya hospitali hiyo pamoja na kumhamisha aliyekuwa Kaimu Mkurugenzi wa hospitali hiyo kutokana na kutoridhishwa na hali ya utendaji wa hospitali hiyo.
Ziara hiyo ya ghafla ya Rais Magufuli pia ilibaini kutofanya kazi kwa mashine za MRA pamoja na CT-Scan katika hospitali hiyo huku akielezwa kwamba mashine kama hizo zinafanya kazi vyema katika hospitali za watu binafsi.