KATIBU Mkuu Kiongozi, Balozi Ombeni Sefue ametembelea Hospitali ya Taifa ya Muhimbili (MNH) na kuwasilisha maagizo ya Rais John Magufuli ambayo ni kuwataka madaktari wote nchini, kuhakikisha wanatumia muda wao kazini na si kufanya mambo yao binafsi.
Pamoja na kuuagiza uongozi wa hospitali hiyo kuhakikisha mashine za MRI na CT-Scan, zinaanza kufanya kazi mara moja, pia amebainisha kuwa Serikali ina mpango wa kuongeza mashine mbili za aina hiyo ili kupunguza mzigo wa wananchi kukosa huduma za vipimo zinazotolewa na mashine hizo.

Akizungumza na waandishi wa habari baada ya kumaliza ziara yake hospitalini hapo Dar es Salaam jana, alisema pamoja na madaktari hao, pia Rais Magufuli, amewataka watumishi wote nchini wa umma, kuwajibika kwa wananchi ikiwamo kuvaa majina yao ili iwe rahisi kwa wananchi kuwatambua pindi inapotokea tatizo. “Naomba niwahakikishie na kuwakosoa wale wote wanaosema kuwa hii ni nguvu ya soda, nawaambie ukweli tutafuatilia na tumeanza kutumia mifumo ya Teknolojia ya Habari (Tehama), kudhibiti mapungufu yanayojitokeza katika utoaji wa huduma kwenye sekta za umma,” alisema Balozi Sefue.
Alisema kwa upande wa madaktari wasiowajibika na kutumia muda wao wa kazi Serikalini kuhudumia wagonjwa wao binafsi, sasa muda wao umefika na atakayebainika atachukuliwa hatua za kinidhamu. Aidha, alisema pia Dk Magufuli amezitaka ofisi zote za umma, kuanzisha madawati ya misaada yatakayotumiwa na wananchi kwa ajili ya kusaidiwa kupata huduma vizuri na kuwasilisha malalamiko yao endapo hawatapatiwa huduma kadri inavyotakiwa.
“Natumia fursa hii kuagiza watumishi wote wa umma, kuvaa majina yao wakati wanatoa huduma kama ilivyo kwa askari jeshi na polisi, ili kurejesha imani kwa wananchi, lakini pia kutoa uwazi na fursa kwa wananchi kuweza kuwatambua wanaowahudumia,” alisisitiza. Balozi Sefue pia aliitaka Bohari Kuu ya Dawa Tanzania (MSD), kuhakikisha inafungua maduka ya dawa katika hospitali zote kuu ili kuwasogezea huduma karibu wananchi, huku akisisitiza kutumika haraka kwa mfumo mpya wa kudhibiti wizi wa dawa za Serikali. “Rais anataka ule mfumo wa kuweka alama kwenye dawa za Serikali ufanyike haraka.
Lakini pia natumia fursa hii kuwaonya wenye maduka ya dawa binafsi watakaothubutu kuuza dawa za Serikali kwani cha moto watakiona,” alisisitiza. Akizungumzia vitanda vilivyonunuliwa na Bunge kutokana na agizo la Rais Magufuli la kutumia kiasi cha fedha zilizochangwa kwa ajili ya hafla ya kuzindua Bunge, Balozi Sefue alisema tayari vitanda hivyo vimewasili Muhimbili na wagonjwa wote waliokuwa wanalala chini sasa wamepatiwa vitanda hivyo.
Hata hivyo, alisema amebaini kuwa tatizo hospitalini hapo, halikuwa ni upungufu wa vitanda pekee, ila kulikuwa hakuna wodi za kutosha kulaza wagonjwa, ndio maana wagonjwa wengi hasa wa Taasisi ya Tiba ya Mifupa, Upasuaji wa Ubongo na Mishipa ya Fahamu (MOI) walikuwa wanalazwa chini katika wodi nyingine hospitalini hapo. Alisema tayari taasisi hiyo inatarajia kukamilisha jengo lake jipya na la kisasa ambalo pamoja na kuwa na wodi, pia litakuwa na huduma za vipimo vya MRI na CT-Scan, hali itakayosaidia pia kupunguza matatizo ya vipimo hivyo hospitalini hapo.
Aidha, Sefue alitumia fursa hiyo kuzitaka hospitali zote nchini, kuhakikisha kuwa zinatengeneza mfumo bora wa kufanyia marekebisho mashine zote zinazotumika katika huduma za afya na kuepuka kutupia mzigo wa gharama za matengenezo hayo Wizara ya Afya na Ustawi wa Jamii.
“Kuanzia sasa mikataba yote ambayo taasisi za umma zitaingia kwa ajili ya ununuzi wa vifaa au mashine zinazotoa huduma, lazima iwe na kipengele cha kampuni zinazouza vifaa hivyo, kuhakikisha wanatoa elimu kwa wataalamu Watanzania ili kuepuka gharama kubwa za matengenezo,” alisema.
Kwa upande wake, Katibu Mkuu wa Wizara ya Afya na Ustawi wa Jamii, Dk Donan Mmbando, alisema tayari Serikali imeingia mkataba na nchi ya Uholanzi kupitia Kampuni ya Philips kwa ajili ya kuagiza mashine zaidi ya MRI na CT-Scan ambazo zitatumika katika jengo jipya la MOI. “Pia kupitia mapendekezo yetu ya bajeti inayokuja tumeomba tupatiwe kiasi cha Sh bilioni 12, kwa ajili ya kufanyia ukarabati wa maeneo mbalimbali ya kutolea huduma za afya katika hospitali zetu kuu, lengo likiwa ni kuhakikisha kuwa wananchi wanapata huduma bora za afya,” alisisitiza.
Naye Mkurugenzi Mkuu wa MSD, Laurean Bwanakunu alisema tayari wamewasilisha vifaa vyenye thamani ya Sh milioni 251 kwa MNH kupitia MOI ambavyo ni vitanda na magodoro 300, viti maalumu vya wagonjwa 30, vitanda maalumu vya kubebea wagonjwa 30, shuka 1,695 na mablanketi 400.