Katibu Mkuu Kiongozi, Balozi Ombeni Sefue akizungumza na waandishi wa habari leo katika ukumbi wa Taasisi ya Moyo ya Jakaya Kikwete baada ya kufuatilia agizo la Rais John Pombe Magufuli ambaye awali aliagiza wagonjwa wasilale chini. Rais Magufili aliitembelea Hospitali ya Taifa ya Muhimbili (MNH) hivi karibuni na kutoa agizo hilo. Leo Balozi Sefue ameitembelea mashine ya MRI, ST-Scan na Jengo la Taasisi ya Mifupa ya MOI. Akiwa katika ofisi ambako ipo mashine ya MRI na ST-Scan Balozi Sefue amepewa taarifa ya matengenezo ya mashine hizo. 

Katibu Mkuu Kiongozi, Balozi Ombeni Sefue (katikati) akiwa katika Hospitali ya Taifa ya Muhimbili (MNH) ambako amefanya ziara kuangalia utekelezaji wa agizo la Rais John Magufuli kuhusu huduma bora kwa wagonjwa na kutekeleza wagonjwa kutolala chini. Wagonjwa hivi sasa wanalala kwenye vitanda na siyo chini. Kushoto ni Katibu Mkuu wa Wizara ya Afya na Ustawi na Jamii, Dk Donan Mmbando na kulia ni Mkurugenzi wa Taasisi ya Mifupa ya Moi, Othuman Wanin Kiloloma.

 Katibu Mkuu wa Kiongozi (kulia), Balozi Ombeni Sefue akihoji kutokamilika kwa mashine ya MRI kwa wakati baada ya kutembelea chumba ambako mashine hiyo imehifadhiwa. Ofisa anayesimamia utengenezaji wa mashine hiyo, Monica Joseph ameahidi kwamba mashine hiyo itakamilika Alhamisi ijayo. 

Mmoja wa mafundi wa mshine ya ST-Scan akitoa maelezo kwa Katibu Mkuu wa Kiongozi (kulia), Balozi Ombeni Sefue kuhusu utengenezaji wa mashine hizo. Fundi huyo ameahidi kwamba mashine hiyo itakamilika Jumatano.
Picha zote kwa hisani Hospitali ya Taifa ya Muhimbili (MNH).

SERIKALI Kuendelea Kuboresha Sekta ya Afya Nchini

Katibu  Mkuu  Kiongozi  Balozi Ombeni  Sefue leo amefanya ziara katika Hospitali ya Taifa Muhimbili (MNH) pamoja na mambo mengine amesema serikali itaendelea kuboresha sekta ya afya nchini ili kuhakikisha wananchi wanapata huduma bora na kwa wakati.

Akizungumza baada ya kutembelea MNH, Balozi Sefue amesema  amekagua mashine za MRI na CT-SCAN  na kueleza kuwa spea zimeshafika na kazi ya kutengeneza mashine hizo inaendelea. Pia amesema kwamba Serikali ya Tanzania imesaini mkataba mpya na Serikali ya Uholanzi wa kununua vifaa vipya na Hospitali ya Muhimbili itapata CT-SCAN moja wakati Hospitali ya Bugando itapata mashine moja ya MRI.

Pia,  amewataka wahudumu wa afya kuwahudumia vizuri wagonjwa wanaotumia Bima ya Afya ili kuongeza mapato katika hospitali za serikali.

Akizungumzia kuhusu kudhibiti wizi wa dawa za serikali, Balozi Sefue amesema ni vema ukaimarishwa mfumo wa MSD kwa kutumia mifumo ya Tehama  na kuwa na maduka yao ya ndani.

Katika ziara hiyo, Balozi Sefue amepata fursa ya kufanya kikao na Katibu Mkuu wa Wizara ya Afya Dk Donan Mmbando  na  watendaji wa MNH  ili kupata sura ya matatizo yote katika hospitali hiyo.