UTENDAJI wa Rais John Magufuli unaendelea kuwavutia watu wengi na hatua yake ya kufuta shamrashamra za sikukuu ya Uhuru, imepongezwa kuwa itaokoa fedha za walipa kodi, huku watendaji wa serikali wakianza kutekeleza agizo la kufanya usafi siku hiyo ili kukabiliana na kipindupindu.
Juzi Dk Magufuli aliwataka Watanzania popote walipo kusherehekea sikukuu ya Uhuru, Desemba 9, 2015 kwa kufanya kazi. Kwa mujibu wa Ikulu, maadhimisho ya Uhuru ya mwaka huu yatatumika kama kichocheo cha kujenga tabia ya kufanya kazi (Uhuru na Kazi) nchini.

“Mheshimiwa Rais ameelekeza Watanzania wote siku hiyo waitumie kwa kufanya kazi mbalimbali kama vile, mashambani, maofisini, sokoni, viwandani na usafi wa miji yao katika kutimiza dhana ya Uhuru na Kazi kwa vitendo,” ilisema taarifa hiyo Mhadhiri wa Chuo Kikuu cha Mtakatifu Augustine, Profesa Mwesiga Baregu alisema siku ya Uhuru haina tatizo, tatizo liko kwenye mfumo wa Serikali wa kuwa na matumizi makubwa ya fedha kwenye sherehe kama hiyo na akapongeza hatua ya Rais kufuta shamrashamra hizo.
“Rais aendelee kubana matumizi kwenye sherehe kama hizi, lakini asiifute siku yenyewe maana iko kikatiba. Anaweza akaweka kiasi cha fedha ambacho kinatakiwa kutumika na sio kuwaachia huru watendaji serikalini ambako kuna mfumo mbaya wa matumizi ya fedha za umma,” alisema Profesa Baregu. Msomi na mwanasiasa huyo wa upinzani alimuunga mkono Rais kuondoa fedha za dhifa za Kitaifa, lakini akashauri kwamba kwa sikukuu ya Uhuru ambayo iko kikatiba ni vyema ziruhusiwe baadhi ya shughuli ambazo zitaienzi siku hiyo badala ya kuiondoa kabisa.
Hata hivyo, serikali katika taarifa yake ilisema kuwa sherehe hizo zitaendelea mwaka kesho kama ilivyozoeleka na kusisitiza kwamba haiwezekani Watanzania wakasherehekea miaka 54 ya uhuru huku wenzi wao wakifa kwa kipindupindu. Mwenyekiti wa Jukwaa la Katiba, Deus Kibamba akielezea utendaji wa Dk Magufuli, alisema anaona ameanza vizuri kwa kuwapa matumaini wananchi na akaomba asilegeze kamba kuhusu misimamo yake.
Kibamba alishauri Dk Magufuli apewe nafasi ya kutekeleza ndoto zake licha ya kuwa mabadiliko anayotarajia kufanya yanaweza kuchukua muda mrefu. Hata hivyo, Kibamba alishauri rais amalizie pia mchakato wa kuundwa kwa Katiba mpya ambao uliachwa njiani huku kukiwa na mgawanyiko mkubwa. Pia alisema Dk Magufuli aendelee na vita dhidi ya rushwa na ufisadi pamoja na utoaji wa haki kwa makundi ambayo yanakandamiziwa.
“Kama alivyoanza yeye mwenyewe, hata baraza lake la mawaziri ambalo ataliunda liwe na dhamira ya dhati ya kupambana na rushwa,” alisema. Kibamba pia alishauri Rais asiwe na msamaha kwa wote wanaokwepa kodi. “Natamkia kila la heri katika kipindi hiki ambacho yuko kwenye mchakato wa kuunda baraza lake la mawaziri na aendelee kuleta mageuzi makubwa katika usimamizi wa rasilimali za umma,” alisema.
Mhadhiri wa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam, Dk Frank Tily, alisema kuleta mageuzi sio jambo rahisi hasa katika mfumo huu ambao kuna watu wachache wanafaidika. Akasema anatakiwa apate msaada kutoka kwa wasaidizi wake ili afikie malengo yake. Alisema kuna haja pia ya kuboresha maslahi ya wafanyakazi ili yakidhi wakati na wafanye kazi kwa kasi anayotaka. Alimshauri pia Rais Magufuli kuwa na vipaumbele vichache kama anataka kuleta maendeleo kwa haraka.
Mhadhiri wa Chuo Kikuu Huria (OUT), Emannuel Mallya, alisema Rais Magufuli alipoanzia ni pazuri na akaomba na akashauri aunde mifumo ambayo itasaidia kusukuma mbele maono yake. “Rais kwa sasa mpango wake ni kuunda baraza la mawaziri, anaweza kuteua watu ambao watamsaidia kujenga mifumo ambao watapanga na kutekeleza mawazo na ndoto zake za Tanzania aitakayo,” alisema Malya.
Mjini Bukoba, siku moja baada ya agizo la Dk Magufuli, Serikali ya Mkoa wa Kagera imeanza kutekeleza agizo hilo la usafi kwa vitendo ikiwamo kufunga migahawa. Mkuu wa Mkoa wa Kagera, John Mongella alizindua kazi hiyo jana katika Manispaa ya Bukoba kwa kufanya usafi katika mitaa mbalimbali na kikosi kazi cha watendaji wa Manispaa hiyo na vyombo vya ulinzi. Mpaka jana kulikuwa na wagonjwa 26 wa kipindupindu mkoani humo huku watu wawili wakiaminika kupoteza maisha kwa ugonjwa huo.
Katika ‘Operesheni tokomeza kipindupindu Kagera’, Mongella alimuagiza Ofisa Afya wa Manispaa, Ladislaus Oisso kufunga migahawa na vilabu vya pombe za kienyeji ambavyo mazingira yake ni machafu kwa muda usiojulikana. Alisema watakaokaidi agizo hilo, wakikamatwa watatozwa faini ya Sh 50,000 kila mmoja. Maeneo yaliyohusika na operesheni hiyo ambapo mkuu huyo alitembelea kwa miguu huku akishirikiana na wananchi kufanya usafi ni kata za Bakoba, Kashai, Miembeni na Bilele zilizo katika Manispaa ya Bukoba.
Pia aliagiza maofisa afya wote kuzibua mitaro, kuondoa na kuzoa taka ngumu zilizopo katika maeneo mbalimbali mkoani humo. “Kipindupindu ni ugonjwa ambao unaenea kutokana na watu kula vyakula vyenye bakteria waliochang’anywa na kinyesi, kwa hiyo dawa ya kuzuia kipindupindu ni kuondokana na uzembe na kufanya usafi kwa kushirikiana katika maeneo yetu, hivyo hatuna budi kutambua kuwa wakati huu ni kuhakikisha tunafanya usafi katika mazingira yetu, kwa hili hakuna mzaha.
Atakayekaidi atachukuliwa hatua,” alisema Mongella. Alitoa agizo kuwa ifikapo Desemba mosi mwaka huu ugonjwa huo uwe umemalizika katika maeneo yote ya mkoa huo na endapo katika nyumba yoyote atapatikani mgonjwa wa kipindupindu baada ya tarehe hiyo, wahusika watafungiwa huduma na kuwekwa katika karantini kwani sheria inayoruhusu kufanya hivyo ipo.
Pia Mongella aliagiza kuwa maeneo yote yaliyofungwa hasa migahawa na vilabu za pombe za kienyeji (vigata) hakuna kufunguliwa na mtu yeyote mpaka Serikali ya Mkoa itakapojiridhisha na kutoa maelekezo upya. Aidha, alivitaka vikosi kazi vilivyoundwa katika maeneo mbalimbali vinavyowashirikisha polisi, mgambo na watendaji wa Manispaa kupita kwa wananchi kuwapatia elimu juu ya suala la usafi ambalo ni agizo la Rais Magufuli na wala siyo kwenda kwa wananchi na kuwatisha.
Aliagiza pia kwamba kila Alhamisi itakuwa siku ya usafi. Naye Mkuu wa Wilaya ya Bukoba, Jackson Msome alisema Serikali imeshtushwa na ongezeko la haraka la wagonjwa 10 ndani ya saa 24 ambapo Novemba 22, mwaka huu walikuwa 16, lakini juzi wameongezeka hadi kufikia 26. Imeandikwa na Shadrack Sagati, Dar na Angela Sebastian, Bukoba.