Mkurugenzi wa Usimamizi wa Elimu Ofisi ya Rais,Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (Tamisemi), Juma Kaponda
WAKATI Serikali ikipambana ili wanafunzi wapate mazingira bora ya kujifunzia, kwa kuhakikisha kunakuwa na madawati, maabara, vitabu na sheria ngumu kwa watakaooa au kuwapa ujauzito wanafunzi, utafiti umebaini kuwa asilimia 51 ya walimu nchini ni watoro.

Utafiti huo uliofanywa na wadhibiti ubora wa elimu katika shule mbalimbali, umebaini kuwa asilimia 51 ya walimu nchini, hawafundishi wanafunzi wakati wa saa za kazi.
Mkurugenzi wa Usimamizi wa Elimu Ofisi ya Rais,Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (Tamisemi), Juma Kaponda, alisema hayo juzi wakati akifungua mafunzo ya siku tatu ya uwezeshaji wa wawezeshaji wa kamati za shule 528, wanaotoka katika halmashauri 123 za mikoa 19 nchini nzima.
Kwa mujibu wa Kaponda, utafiti huo uliofanyika katika miezi ya hivi karibuni, ulibaini ni asilimia 49 tu ya walimu waliopo kazini wanafundisha na hao asilimia 51 hawafundishi na baadhi yao kama wakifundisha, ni kwa muda tu na kuondoka kwenda kufanya shughuli nyingine.
Kutokana na udhaifu huo, Kaponda amewaagiza maofisa elimu wa mikoa, ofisa taaluma wa mikoa na wenzao wa ngazi hizo katika wilaya, kuanza kufuatilia walimu shuleni kuona kama wanawajibika kufundisha madarasani.
Alisema kitendo cha walimu kutofundisha wanafunzi madarasani kwa muda uliopangwa na kupokea mishahara, ni sawa na kuwa mfanyakazi hewa anayeiibia fedha serikali.
“Walimu wapo wengi, lakini wanaofundisha ni wachache kwa sasa ni lazima sisi viongozi tufanye kazi ya kusimamia maadili ya walimu, ufundishaji na kuhakiki ubora wa kiwango cha taaluma na wale wazembe hatua stahiki zichukuliwe kwa mujibu wa sheria za utumishi wa umma,” alisema Kaponda.
Kaponda alisema mwalimu asiyefundisha kwa muda mrefu hata kama alikuwa ni mzuri kwa kiwango cha juu, uwezo wake hupungua na kurudisha nyuma kiwango cha taaluma katika shule husika. Katika hatua nyingine, serikali imetoa Sh bilioni 15 kwa ajili ya gharama za Julai za uendeshaji wa shule zote za msingi na sekondari nchini.
Kaponda amesema tayari fedha hizo zimepokewa Tamisemi na taratibu za kuingizwa katika akaunti za shule husika umeshakamilishwa kwa ajili ya matumizi ya uendeshaji wa shule kwa mujibu wa utaratibu uliopo.
Alihadharisha kuwa matumizi ya fedha hizo yafanyike kwa malengo yaliyowekwa na serikali chini ya mwongozo uliotolewa na kwa watakaokwenda kinyume chake, watawajibishwa kwa mujibu wa sheria za utumishi wa umma.