Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu
WATU watatu wakiwemo wanafunzi wawili wa vyuo vikuu vilivyoko jijini Dar es Salaam wamepandishwa kizimbani katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu, Dar es Salaam wakikabiliwa na mashitaka ya mauaji.
Wanafunzi hao ni wa Chuo Kikuu cha Ardhi, Hussein Mustafa (26) na wa Chuo Kikuu Huria (OUT), Haruna Nkuye (24) ambao wanashitakiwa pamoja na fundi makenika Rajabu Ally (41) wote wakazi wa Dar es Salaam.

Washitakiwa hao wanaodaiwa kuhusika na mauaji hayo kwenye tukio la ujambazi katika Benki ya CRDB eneo la Chanika Wilaya ya Ilala, Dar es Salaam, walisomewa mashitaka na Wakili wa Serikali Jackson Chidunda mbele ya Hakimu Mkazi Mkuu Huruma Shahidi.
Akisoma hati ya mashitaka, Chidunda alidai Desemba 8, mwaka jana katika eneo la Chanika, Wilaya ya Ilala, Dar es Salaam, washitakiwa walimuua Ramadhani Halili, Shan Rajabu na Thomas Otemu.
Hakimu Shahidi alisema washitakiwa hawatakiwi kujibu mashitaka kwa kuwa mahakama hiyo haina mamlaka ya kusikiliza shauri hilo isipokuwa Mahakama Kuu.
Upande wa jamhuri ulidai kuwa upelelezi wa kesi hiyo haujakamilika na kuomba tarehe nyingine ya kutajwa ili wamuunganishe mshtakiwa Mohamed Ungando ambaye jana hakuwepo mahakamani.
Awali, mshitakiwa Mustafa aliiomba mahakama imsaidie apate matibabu kwa kuwa viungo vinamuuma kutokana na adhabu alizopewa akiwa mahabusu.
Hakimu Shahidi alisema gerezani kuna utaratibu wa matibabu, kama hatatibiwa kesi itakapotajwa tena aijulishe mahakama. Kesi hiyo imeahirishwa hadi Julai 14, mwaka huu.