Rais John Magufuli na Waziri Mkuu wa India, Narendra Modi wakipiga ngoma ya asili Ikulu, Dar es Salaam jana, baada ya waziri huyo kuwasili nchini kwa ziara ya kikazi. (Picha na Ikulu).
UJIO wa Waziri Mkuu wa India, Narendra Modi umekuwa neema kwa Tanzania kutokana na kusainiwa kwa makubaliano ya mikataba mbalimbali ya uendelezaji sekta mbalimbali huku nchi hiyo ikiahidi kutoa mkopo nafuu wa takribani Sh trilioni moja kwa ajili ya kutekeleza miradi ya kipaumbele nchini.

Nchi hiyo ya Bara la Asia, imesaini mikataba kadhaa ya uendelezaji wa viwanda, kilimo, afya, maji na teknolojia na wakati huo huo kuingia makubaliano ya kuondoa viza kwa wanadiplomasia na watumishi wa umma wanaokwenda nchini humo.
Aidha katika mkutano na waandishi wa habari, uliofanywa na Waziri Mkuu, Modi na Rais John Magufuli, jijini Dar es Salaam jana, kiongozi huyo wa India alisema Magufuli ana maono ya kujenga taifa, ambayo yako pia kwenye ndoto zake kwa ajili ya nchi yake.
“Rais Magufuli ana maono ya kujenga taifa, maendeleo na kuifanya Tanzania ya viwanda, maono ambayo pia yako katika ndoto zangu kwa India,” alisema Modi kwenye mkutano huo na waandishi wa habari.
Kwa upande wake, Rais Magufuli aliwataka watanzania kuchangamkia fursa mbalimbali, zinazotokana na uhusiano wa nchi hizo mbili, ikiwamo kilimo cha mazao jamii ya kunde ambacho nchi hiyo imesaini mkataba wa kukiboresha.
Kuhusu mkopo nafuu, Waziri Mkuu Modi alisema nchi yake inatarajia kuipa Tanzania mkopo nafuu wa dola za Marekani milioni 500, sawa na zaidi ya Sh trilioni moja kwa ajili ya kutekeleza miradi ya kipaumbele hapa nchini. Modi alisema hatua hiyo inatokana na mazungumzo rasmi waliyoyafanya na Rais Magufuli, Ikulu jijini Dar es Salaam.
“… Pia tuna nia ya kusaidia mkopo nafuu wa dola milioni 500 kwa ajili ya mikopo yenye masharti nafuu,” alisema.
Mikataba iliyosainiwa
Mikataba iliyosainiwa ni Mpango mkakati wa pamoja kati ya Shirika la Viwanda Vidogo India (NSIC) na Shirika la Viwanda Vidogo Tanzania (SIDO) kwa ajili ya ushirikiano kwa wajasiriamali wadogo na wa kati.
Pia wamesaini mkataba unaowezesha mpango wa uanzishaji wa vituo vya atamizi (incubators), zitakazosaidia wabunifu kunufaika na mafunzo na teknolojia ya India. Serikali hiyo ya India pia imesaini hati ya makubaliano kuhusu miradi ya usimamizi, uhifadhi na uendeshaji mkataba na makubaliano viwanda vya kati na vidogo.
Hati nyingine za makubaliano ni ya vyuo vya ufundi kati ya India na Zanzibar, ambayo yatasaidia katika ubunifu na mafunzo ya ufundi. India itajenga kituo mahususi kwa ajili ya mafunzo ya ufundi mjini Pemba.
Wakati huo huo, umesainiwa mkataba wa makubaliano ya kuondoa viza kwa wanadiplomasia na watumishi wa umma.
Mengine ni mkopo wa dola za Marekani milioni 92.18 kwa ajili ya kuimarisha usambazaji wa maji Zanzibar. Makubaliano mengine kati ya India na serikali, ni kuinua kilimo cha mazao aina ya mikunde, kusaidia utaalamu kwenye tehama, afya ambako Rais Magufuli amealika uwekezaji kwenye viwanda vya dawa.
Rais Magufuli anena Akizungumza na waandishi wa habari, Rais Magufuli alisema, “kabla ya kuja hapa, tumefanya mazungumzo. Yalikuwa mazuri sana, tumejadiliana masuala mengi ya kuimarisha uhusiano katika ya nchi hizi mbili.”
Kwa upande wa kilimo, nchi hiyo imekubaliana kuimarisha na kuboresha mazao ya jamii ya kunde hususani choroko, dengu na kunde kwa kusaidia teknolojia, mbegu na mbolea muafaka.
Alisema mwaka jana Tanzania iliuza tani 100,000 za mazao hayo yenye thamani ya dola za Marekani milioni 200, wakati nchi hiyo ina mahitaji ya tani milioni saba kila mwaka kwa ajili ya matumizi yake ya ndani. “ Tumekubaliana kuongeza uzalishaji wa mazao na kuingia mkataba wa bei ya mazao hayo ili kuepuka madalali,” alisema Magufuli.
Aliongeza: “Nawaomba watanzania wachangamkie fursa hii kwa kulima mazao haya kwa wingi, kwa sasa soko la uhakika limepatikana bila kupitia madalali, ambao hupanga bei zinazowaumiza wakulima”.
Tehama
Eneo lingine ambayo nchi hiyo imeahidi kusaidia ni kwenye utaalamu wa masuala ya teknolojia ya habari na mawasiliano (Tehama) kwa kusomesha wataalamu wa Kitanzania nchini mwao. “Hili litawezesha nchi yetu kuwa na uwezo wa kutengeneza programu zetu wenyewe, badala ya kununua kutoka nje.Tutaweza kuwa na usiri wa taarifa zetu, usalama wa nchi, utoaji wa huduma na pia kusimamia vizuri ukusanyaji wa mapato kwasababu program zitakuwa ni zetu.”
Viwanda
Eneo lingine la makubaliano ni kushirikiana katika kubadilisha uzoefu na kufanya tafiti kutoka kwenye Shirika la Viwanda Vidogo la India na Sido.
“Tuna furaha ndugu zetu wa India wamekubali Shirika la Viwanda Vidogo kushirikiana na SIDO, katika kubadilishana uzoefu, kufanya utafiti na kutoa ushauri kuhusu miradi na sera ya uendelezaji wa viwanda vidogo,” alisema.
“Naamini ushirikiano huu utatuwezesha kufikia azma yetu ya kuwa nchi ya uchumi wa kati, unaoongozwa na viwanda ifikapo mwaka 2025."
Kimataifa
Magufuli alisema katika harakati za kufanyia mageuzi Baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa, Tanzania imekubali kuiunga mkono India katika kutafuta uwakilishi. Vivyo hivyo India imeahidi kuunga mkono Umoja wa Afrika katika kupata mwakilishi katika baraza hilo. “Natoa mwito kwa taasisi zinazohusika kuhakikisha makubaliano tuliyoyafikia wanayatengenezea mipango kazi mizuri, kwa ajili ya kujiendelezaji,” alisema.
Uwekezaji viwanda
Akizungumzia makubaliano kuhusu sekta ya afya, Rais Magufuli alisema “Tanzania tunatumia asilimia 80 ya fedha zetu katika sekta ya afya kununulia dawa. Na asilimia 100 ya fedha za vifaa tiba zinanunuliwa kutoka nje, hivyo nimemuomba Waziri Mkuu wa India ije iwekeze katika viwanda vya kutengeneza dawa …”.
Alisema pia ameomba wawekezaji wa India waje kuanzisha viwanda vya kuunda pikipiki, bajaj na magari ili isaidie kuongeza ajira kwa Watanzania.
Akizungumzia uhusiano kati ya nchi hizo, Rais Magufuli alisema Tanzania na India, zina uhusiano mzuri na wa muda mrefu uliojengwa katika misingi ya kuheshimiana na maslahi ya pamoja katika ngazi ya kimataifa na kitaifa na kupitia Umoja wa Mataifa, Jumuiya ya Madola na Jumuia ya India-Afrika.
“Ziara hii ni kielelezo cha uhusiano wetu mzuri ambao umeziwezesha nchi zetu kunufaika kiuchumi, hivi sasa India ni mbia wetu mkubwa kibiashara,” alisema.
Thamani ya bidhaa ambazo Tanzania imeuza katika soko la India imeongezeka kutoka dola za Marekani milioni 187 kwa mwaka 2009 hadi kufikia dola za Marekani bilioni 1.29 mwaka 2015. India ni nchi ya tatu yenye uwekezaji mkubwa nchini, ikifuatiwa na Uingereza na China.
Uwekezaji kutoka India ambao umesajiliwa kwenye Kituo cha Uwekezaji Tanzania (TIC), una thamani ya dola za Marekani bilioni 2.4 ambazo zimezalisha ajira zaidi ya 54,176.
“ India tumekuwa tukishirikiana katika masuala ya kijamii, elimu, maji na afya, hivi sasa watanzania wapatao 2000 wako nchini India kwa ajili ya mafunzo mbalimbali. Tangu mwaka jana India imekuwa ikitoa nafasi 330 za masomo kwa watanzania kusomea nyanja mbalimbali. Hivi punde tumeona mikataba iliyosainiwa, lakini pia tumeona faida kubwa ya fedha zilizotolewa karibu milioni 178 kwa ajili ya mradi wa maji Pwani na Dar es Salaam. Hali kadhalika, utiaji saini wa mikataba sita, inayohusu mkopo wa dola za Marekani milioni 92.8 kwa ajili ya usambazaji wa maji Zanzibar."
Msaada mwingine ni wa mashine ya upimaji wa kansa katika hospitali ya Bugando, ambavyo serikali ya India imetoa kwa hospitali. Mashine hii itasaidia kutoa huduma kwa wananchi wa Kanda ya Ziwa na watanzania kwa ujumla.