Mkuu wa Wilaya ya Ikungi Mirajji Jumanne Mtaturu akisisitiza jambo wakati wa kufunga mafunzo
ya waendesha pikipiki.

Mkurugenzi wa Taasisi inayojihusisha na
kupunguza umasikini na kutunza mazingira nchini Tanzania (APEC), Respicius Timanywa akiwashukuru
washiriki wote wa mafunzo hayo



Dc Mtaturu (Kushoto) akimkabidhi Mkurugenzi wa APEC Respicius Timanywa zawadi
ya kuku iliyotolewa na wahitimu wa mafunzo hayo

Mkuu wa Wilaya ya Ikungi Mirajji Jumanne Mtaturu akisisitiza juu ya umuhimu wa mafunzo ya usalama
barabarani.

Dc Mtaturu akionyesha kuku aliyokabidhiwa kama zawadi
baada ya kukubali kuwa mgeni rasmi  wakati wa kufunga mafunzo hayo

Baadhi ya washiriki wa mafunzo ya elimu ya usalama
barabarani wakionyesha alama za barabarani walizozichora wao wenyewe kwa ajili
ya kuashiria kuelewa mafunzo waliyopatiwa



Baadhiya Bodaboda za washiriki zikiwa zimepaki bila
kufanya kazi ya kubeba abiria ambapo wamiliki walikuwa kwenye mafunzo









Na Mathias Canal, Singida



Serikali imeeleza kuwa ipo tayari kuchukiwa na wananchi wavivu wasiotaka
kujishughulisha na Ujasiriamali, Kilimo, Uvuvi, Ufugaji na Biashara ili kukuza
pato la kaya zao.



Hayo yamesemwa na Mkuu wa Wilaya ya Ikungi Mhe Miraji Jumanne Mtaturu wakati wa kufunga mafunzo ya usalama
Barabarani kwa Waendesha pikipiki maarufu kama Bodaboda wa Wilaya ya Ikungi
yaliyohusisha Kata ya Issuna na na Kata ya Mkiwa na kufanyika JMC Hotel
Kijijini Issuna B.



Katika mafunzo hayo yaliyochukua siku sita yamewakutanisha pamoja waendesha
Bodaboda 84 ambao wamefundishwa Alama na sheria zote za usalama Barabarani,
Upatikanaji wa leseni, Faida za kulipa kodi na somo la ujasiriamali, Polisi
jamii, Ulinzi shirikishi na elimu juu ya maambukizi ya Virusi Vya Ukimwi (VVU)
na Ukosefu wa Kinga Mwilini (UKIMWI).



Akiwahutubia wananchi hao Mtaturu amemshukuru Rais wa awamu ya nne Dkt Jakaya Mrisho Kikwete kwa kuanzisha
ajira ya pikipiki kwani kwa kiasi kikubwa imesaidia kupunguza uhalifu na
kuandaa ajira kwa vijana wengi nchini hivyo kuachana na kujihusisha na mambo
yasiyo na tija kwa jamii ikiwemo kushinda vijiweni.



Amesema kuwa mafunzo hayo yanayotolewa na shirika lisilo la kiserikali la
APEC yatasaidia kupunguza ajali za pikipiki zinazosababishwa na uzembe wa
baadhi ya waendesha pikipiki katika Wilaya zote za Mkoa wa Singida.



Dc
Mtaturu
amemwagiza Mkurugenzi wa Halmashauri ya Wilaya ya Ikungi
kwa kushirikiana na Mkuu wa Polisi Wilaya kuhakikisha madereva Bodaboda waliokwepa
mafunzo ya awamu hii wanasajiliwa ili
wahudhurie mafunzo yatakayorudiwa kwa awamu ya pili kwa Wilaya nzima, hivyo kwa
wale ambao hawatapata mafunzo hawataruhusiwa kuendesha pikipiki zao ili
kuepusha ajali mpaka pale watakapopata mafunzo.

“Dereva bila elimu ni sawa na bunduki bila risasi,
hivyo nakuagiza mkuu wa Polisi kutowakamata kwa kosa la kutokuwa na leseni
angalau kwa kipindi cha miezi miwili wakati wanafuatilia leseni zao”  Alisema
Mtaturu

Akizungumzia kuhusu alama za barabarani Mtaturu
alisema kuwa tayari ameshamwagiza Mhandisi wa Ujenzi wa Halmashauri kufanya
mawasiliano na wakala wa barabara katika maeneo yote ambapo alama za barabarani
hazipo.

Ili kuvunja makusudi makusudi ya kuvunja sheria Mkuu
huyo amemuagiza Mkuu wa Polisi Wilaya (OCD) amuelekeze mkuu wa Trafiki Wilaya
(DTO) ambapo alisema kuanzia leo kila dereva wa pikipiki anapaswa kutembea na
kivuli cha cheti na leseni. 

Akisoma risala iliyoandaliwa na wahitimu wa mafunzo
ya udereva wa pikipiki Kata ya Mkiwa na Issuna Yohana Chawenda amezitaja changamoto zinazowakabili waendesha
bodaboda hao kuwa ni pamoja na kukabwa na kuibiwa pikipiki zao, Upatikanaji wa
leseni, baadhi ya abiria kukataa kuvaa kofia ngumu, Baadhi ya waendesha
pikipiki kukataa kushiriki mafunzo ya usalama barabarani, Baadhi ya wananchi
kuharibu alama za barabarani na Baadhi ya maafisa wa usalama Barabarani
kusimamisha pikipiki sehemu isiyo rasmi jambo ambalo linachangia kuongezeka kwa
ajali za barabarani.

Mkurugenzi wa Taasisi inayojihusisha na kupunguza
umasikini na kutunza mazingira nchini Tanzania (APEC), Respicius Timanywa, amesema kuwa lengo la Taasisi hiyo kutoa mafunzo hayo ni kupunguza ajali na
kuwaandaa vijana kujihusisha na ujasiliamali wa uendeshaji wa Bodaboda huku
wakiwa katika hali ya usalama.

Timanywa amesema kuwa mafuzno hayo yataendelea
katika maeneo mengine ili kutoa fursa kwa watanzania wote wanaopenda kushiriki
kwa ajili ya kujifunza kwa manufaa ya leo na kesho.

Zaidi sana amesema kuwa mafunzo hayo pia yamelenga
kuwafanya vijana waweze kumiliki fursa kubwa na kutengeneza faida kubwa iliwaweze
kulipa ushuru na kodi za serikali.