Mchungaji
LILE andiko la usimjaribu bwana Mungu wako lililosemwa na Yesu Kristu limejidhihirisha baada ya mchungaji maarufu nchini Afrika Kusini, Alfred Ndlovu (44), kufariki dunia baada ya kufunga usiku na mchana kwa takribani siku 30 akitaka kuvunja rekodi ya Yesu Kristu aliyefunga siku 40 bila kula kitu chochote.
Kama alivyofanya Yesu Kristu, Mchungaji Ndlovu naye aliondoka nyumbani kwake Juni  17 mwaka huu na kuelekea nyikani kwa ajili ya kufunga na kuomba, huku akiweka pembeni anasa za dunia.
Kifo cha mchungaji huyo kimeishangaza sana familia yake, waumini wa kanisa lake na jamii nzima kwa ujumla.
Mchungaji huyo alijulikana kwa imani yake thabiti ambayo  ingeweza hata kuhamisha milima.
Mmoja wa wanafamilia ya mchungaji huyo alisikika akilalamika; “Alikuwa mtu wa imani sana. Lakini kwa bahati mbaya amefariki kifo hicho. Baada ya mwezi ndipo tumepata taarifa za kifo chake”
Akijaribu kuvunja rekodi ya Yesu, Mchungaji Ndlovu alifariki baada ya kufunga kwa takribani siku 30 japokuwa hakuwahi kuripotiwa kuwa na ugonjwa wowote hapo awali. Alikuwa peke yake nyikani na maiti yake iligunduliwa na mpita njia mmoja aliyetoa taarifa polisi.