Kamanda wa Polisi Mkoa wa Kilimanjaro, Wilbroad Mutafungwa
MFANYABIASHARA mmiliki wa Shule ya Sekondari ya Merinyo wilayani hapa, Roman Shirima (74) amejiua baada ya kujimwagia mafuta ya petroli kisha kujiwasha moto, hali iliyosababisha kuungua hadi kufa.

Akitoa taarifa za tukio hilo, Kamanda wa Polisi Mkoa wa Kilimanjaro, Wilbroad Mutafungwa alisema mfanyabiashara huyo alijiua Agosti 18, saa 11:25 alfajiri nyumbani kwake eneo la Mjohoroni Kata ya Msaranga Ng’ambo, Manispaa ya Moshi.
Kamanda Mutafungwa akielezea mazingira ya kifo hicho, alisema siku ya tukio mfanyabiashara huyo alichukua mafuta ya petroli na kujimwagia mwili mzima, kisha kujiwasha na kiberiti, hali iliyomfanya aungue vibaya na kusababisha kifo chake papo hapo.
Alisema chanzo cha tukio hilo hakijajulikana na kwamba jeshi hilo linaendelea na uchunguzi ili kubaini chanzo cha mfanyabiashara huyo kujiua mwenyewe. Mwili wa marehemu umehifadhiwa katika Hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa Kilimanjaro, Mawenzi kusubiri taratibu za mazishi.