Bomu kubwa la kutegwa ndani ya gari limelipuka kwenye makao makuu ya polisi wa kutuliza ghasia mjini Cizre, kusini mashariki mwa Uturuki na kuwauwa polisi 11, na wengine 70 wamejeruhiwa
Haijafahamika ni nani aliyetekeleza shambulio hilo, lakini vyombo vya habari vya Uturuki vimelaumu chama cha wafanyakazi wa kikurdi kilichopigwa marufuku cha -PKK - kuhusika na shambulio hilo.

Wakazi wa mji wa Cizr wamekuwa chini ya tahadhari ya kutotoka nje kwa miezi kadhaa iliyotangazwa na mamlaka za Uturuki zinazopigana dhidi ya PKK.
Shrika la Umoja wa Mataifa la haki za kibinadamu limedai uchunguzi ufanyike kuhusu madai ya kwamba watu zaidi ya 100waliteketezwa kwa moto hadi kufa walipokuwa wamewomba hifadhi kwenye chumba cha chini ya ardhi mjini Cizre - mji wenye umskini uliopo mpakani na Syria.
Serikali ya Uturuki imepinga madai kwamba raia walilengwa na mashambulio hayo.
Vikosi vya usalama vya Uturuki vimekua vikiendesha misururu ya mashambulio dhidi ya PKK tangu kuvunjwa kwa mkataba wa miaka miwili wa usitishaji mapigano wa mwezi Julai mwaka 2015.
tangu wakati huo, harakati za kijeshi kusinini mashariki mwa nchi zimekuwa zikiendelea PKK wakilipiza kisasi ambapo mamia ya watu wameuawa.
Mzozo wa PKK nchini Uturuki unaonyesha ishara ya kusambaa kote nchini anasema mwandishi wa BBC Mark Lowen, na serikali imekataa mashautriano yoyote hadi pale kundi hilo litakaponyang'anywa silaha zote.
Ghasia za hivi punde zinatokea wakati jeshi la Uturuki likijihami vilivyo kufuatia jaribio la mapinduzi la mwezi Julai.
sambamba na wapiganaji wa PKK, Uturuki inapigana na Islamic State, ambalo wapiganaji wake waliendesha msururu wa mashambulio ya umwagaji damu katika kipindi cha mwaka uliopita.
PKK, ambacho kimepigwa marufuku nchini Uturuki , kilianza mashambulizi yake mnamo mwaka 1984, kikidai kupinga mamlaka za Uturuki kuwabagua na kuwatesa wakurdi.