Mwenyekiti wa THBUB, Bahame Nyanduga
TUME ya Haki za Binadamu na Utawala Bora (THBUB) imekishauri Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA), kusitisha maandamano yake ili kutoa nafasi kwa mahakama kufanya kazi yake kwa umakini bila shinikizo la muda kati ya sasa na Septemba mosi mwaka huu.
Aidha, imelishauri jeshi la Polisi kutotumia neno ‘tutawashughulikia wote watakaokaidi amri’ kwa kuwa imeona maneno hayo yanaweza kusababisha matumizi mabaya ya mamlaka ya jeshi hilo.

Katika hatua nyingine, Mahakama Kuu imetupilia mbali maombi ya wadhamini wa Chadema ya kupinga amri iliyotolewa na Mkuu wa Jeshi la Polisi, Inspekta Jenerali (IGP) Ernest Mangu ya kupiga marufuku mikutano ya kisiasa kwa muda usiojulikana.
Mwenyekiti wa THBUB, Bahame Nyanduga aliyasema hayo jana Dar es Salaam wakati akizungumza na waandishi wa habari baada ya kumalizika kwa mkutano uliohudhuriwa na Msajili wa Vyama vya Siasa nchini, Jaji Francis Mutungi, Katibu Mkuu wa Chadema, Dk Vincent Mashinji na washauri wake pamoja na Mkurugenzi Mtendaji wa Taasisi ya Demokrasia Tanzania (TCD), Daniel Loya.
Nyanduga alisema Tume iliandaa mkutano huo ili kuzungumzia tamko la jeshi la Polisi la Juni 7, mwaka huu la kuzuia mikutano na maandamano ya vyama vya siasa isiyo ya kiutendaji na tamko la Chadema kuhusu Operesheni ya Umoja wa Kupambana na Udikteta Tanzania (UKUTA) na mikutano wanayopanga kufanya Septemba mosi, mwaka huu.
Alisema mkutano huo wa jana ulikuwa na lengo la kuwakutanisha viongozi wa Serikali, jeshi la Polisi na Chadema na kwa pamoja kutafuta ufumbuzi wa kile Tume inachohofia kuhusu uvunjifu wa amani, haki za binadamu na utawala bora.
Aidha, alisema baada ya tamko la Chadema la kufanya maandamano nchi nzima, kumekuwa na matamko mbalimbali kutoka kwa viongozi wa kitaifa, baadhi ya wakuu wa mikoa na wilaya, makamanda wa mikoa wa jeshi la Polisi kukataza kufanyika kwa maandamano hayo na kwamba watakaokiuka zuio hilo ‘watashughulikiwa.’
“Ni katika mazingira haya, Tume imepata wasiwasi kuwa endapo matamko haya yataachwa yaendelee, yana viashiria vya machafuko na uvunjifu mkubwa wa haki za binadamu unaoweza kutokea. Mkutano huo ulitaka kujihakikishia iwapo Tume ina mamlaka ya kujadili hoja hizo mbili za zuio la maandamano na mikutano ya vyama vya siasa visivyokuwa vya kiutendaji na kuhusu lugha na matamshi yasiyostahiki,” alisema Nyanduga.
Alisema baada ya majadiliano hayo, wajumbe wote waliohudhuria kikao hicho walikubaliana kuhusu umuhimu wa kudumisha amani nchini na umuhimu wa kuwepo majadiliano katika kutafuta maafikiano ya tofauti zozote kila mara zinapojitokeza na walipendekeza umuhimu wa kuendelea na majadiliano yaliyoanzishwa na Tume.
“Kuhusu mustakabali wa maandamano na mikutano ya vyama vya siasa ilibainika kuwa kuna kesi mbili zilizofunguliwa na Chadema katika Mahakama Kuu, Masijala ya Dar es Salaam na Mwanza na kesi zote zinaendelea. Kwa kuzingatia Ibara ya 131(2)(a) ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, 1977 inaamini kwamba tafsiri sahihi ya zuio lililotolewa na polisi litapatikana mahakamani,” alisema Mwenyekiti huyo wa Tume ya Utawala Bora na Haki za Binadamu.
Alisema Tume inaamini kwamba Mahakama itayapa mashauri hayo kipaumbele kama ilivyofanya wakati wa kusikiliza kesi ya mita 200 Oktoba mwaka jana ili tafsiri yake ipatikane mapema.
Alisema pamoja na uamuzi huo, kwa kuzingatia mamlaka ya Tume chini ya Ibara 130(1)(g) na (h) ya Katiba ya nchi, kuhusu kutoa ushauri na kutafuta maelewano kati ya viongozi wa Serikali na Jeshi la Polisi kwa upande mmoja na uongozi wa Chadema, Tume imewaasa viongozi wa pande hizo kuacha maneno yanayoashiria uvunjifu wa amani.
“Tunawashauri kusitisha matumzi ya lugha au maneno yenye viashiria vya uvunjifu wa amani, haki za binadamu na utawala bora kwani lugha hizo hazikidhi matakwa ya haki za binadamu, wala utawala wa sheria,” alieleza Nyanduga.
Aidha, alisema tayari kuna mashauri mawili yaliyopo mahakamani ambayo yatawezesha Mahakama kutoa tafsiri ya uhalali wa zuio la Jeshi la Polisi la Juni 7, mwaka huu kuhusu maandamano na mikutano ya vyama vya siasa.
“Tume inashauri kwamba pande zote mbili ziheshimu Mahakama na ziache kutoa matamko ambayo yanaendelea kuongeza joto kuhusu uwepo au kutokuwepo maandamano na mikutano Septemba mosi mwaka huu,” alifafanua.
Pia aliwashauri Chadema kurekebisha msamiati wa mikutano wanayopanga na kuondoa neno ‘Udikteta’ katika mikakati yao ya kisiasa, kwani Tanzania ni nchi yenye taasisi za kidemokrasia na inaheshimu utawala wa sheria na ndiyo sababu Chadema wamekwenda mahakamani.
“Iwapo ushauri huu hautazingatiwa, Tume inatahadharisha kwamba kuna uwezekano mkubwa wa kuwepo na uvunjifu wa haki za binadamu na iwapo itatokea hivyo wahusika wote pia itabidi wawajibike,” alionya.
Hata hivyo, alipoulizwa baadhi ya wajumbe muhimu kutokuwepo katika mkutano huo, Mwenyekiti huyo alisema wote walipewa taarifa ila Polisi na Ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali walitoa taarifa kwa nini wameshindwa kufika kwenye mkutano huo.
“Pia Chama Cha Mapinduzi (CCM) walialikwa lakini hawakufika, hivyo wao na wengine ambao hawakufika mnaweza kuwahoji nyie kwanini hawakufika,” alisema.
Katika Mahakama Kuu, Jaji Kiongozi Ferdinand Wambali alikataa maombi ya wadhamini hao wa Chadema baada ya kukubaliana na hoja za kupinga zilizowasilishwa na IGP na Mwanasheria Mkuu wa Serikali (AG) na kutetewa kortini hapo na Mwanasheria Mkuu Mwandamizi, Gabriel Malata na Mwanasheria Mwandamizi, Haruni Matagane.
Katika pingamizi zao, IGP na AG walieleza kuwa maombi yanayoombwa na walalamikaji hayakuwa yamekamilika na kinyume cha sheria kwa kushindwa kwa Wadhamini wa Chadema kufuata taratibu nyingine zilizopo kabla ya kufungua kesi mahakamani.
Katika uamuzi wake, Jaji Kiongozi alibainisha kwamba walalamikaji walikuwa na fursa ya kufuata taratibu nyingine, kwa kupeleka malalamiko yao dhidi ya IGP kwa Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi kabla ya kwenda kuomba zuio la mahakama. Alisema fursa hizo zinapaswa kufuatwa kwanza kabla ya kuomba mahakama iingilie kati.