NDEGE mpya moja kati ya mbili ya Shirika la Ndege (ATCL) kwa mara ya kwanza imeruka, ikiwa ni sehemu ya kufanyiwa ukaguzi kabla ya kuanza rasmi safari zake.
Ndege hiyo aina ya Bombardier Dash 8-Q400 iliruka saa 9:20 alasiri kutoka katika Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Julius Nyerere (JNIA), Dar es Salaam tayari kwa safari ya kuelekea mkoani Kigoma na baadaye Mwanza.

Marubani wa Kitanzania wakishirikiana na marubani wa kutoka Canada waliokuja na ndege hiyo kwa mara ya kwanza, walirusha ndege hiyo ikiwa ni hatua ya kufanyiwa ukaguzi na Mamlaka ya Usafiri wa Anga Tanzania (TCAA).
Akizungumza kabla ya kuruka na ndege hiyo, Meneja wa Kitengo cha Dharura, John Chaggu alisema ndege hiyo inaruka kwa mara ya kwanza kwa majaribio na kufanyiwa ukaguzi kabla ya kuruhusiwa rasmi na TCAA.
“Juzi tulifanyiwa ukaguzi wa kuangalia namna ya kuwahudumia abiria na inapotokea dharura jinsi gani tutawahudumia na kuhakikisha wako salama, hatua hiyo tumefaulu vizuri sana. Hii ya leo (jana) siyo ndege ya kibiashara, hatutabeba abiria wa aina yeyote zaidi ya watu wachache ambao wanahusika katika kufanya ukaguzi huu. Hii ya leo (jana) tunakwenda Kigoma baada ya hapo Mwanza halafu tunarudi tena Dar es Salaam,” alisema Chaggu.