Rais wa Tanzania Dkt. John Magufuli ameagiza viongozi wote wa Serikali walioalikwa kuhudhuria sherehe za Kilele cha Mbio za Mwenge wa Uhuru kitaifa kutohudhuria sherehe hizo.
Ameagiza wale ambao walishalipwa fedha ya posho na safari kwa ajili hiyo wazirejeshe.

Sherehe hzo zimepangiwa kufanyika tarehe 14 Oktoba, 2016 katika Wilaya ya Bariadi Mkoani Simiyu, kaskazini magharibi mwa Tanzania.
Katibu Mkuu Kiongozi Balozi John Kijazi amesema kupitia taarifa kwamba Rais Magufuli ametoa maagizo hayo ikiwa ni utekelezaji wa azma ya Serikali ya awamu ya tano ya kubana matumizi yasiyo ya lazima na kuelekeza rasilimali nyingi katika shughuli za maendeleo ya nchi.
Viongozi waliotakiwa kufuta safari zao za kwenda Bariadi ni pamoja na Wakuu wote wa Mikoa, Wakuu wote wa Wilaya, Wakurugenzi wote wa Mamlaka za Serikali za Mitaa, Mameya na Wenyeviti wote wa Halmashauri za Majiji, Manispaa, Miji na Wilaya pamoja na watumishi ambao huambatana nao wakiwemo madereva na wasaidizi wao.
Inakadiriwa kwamba idadi ya waliotakiwa kufuta safari ni takriban 1,500.
Viongozi wote wa Mikoa na Wilaya watekakiwa kubaki katika maeneo yao ya kazi na kujiwekea utaratibu wa jinsi ya kuienzi siku ya Kumbukumbu ya Muasisi wa Taifa na Baba wa Taifa Hayati Mwalimu Julius Kambarage Nyerere aliyefariki dunia miaka 17 iliyopita.