Spika wa Bunge, Job Ndugai
SPIKA wa Bunge, Job Ndugai amefanya mabadiliko ya wajumbe wote 24 wa Kamati ya Bunge ya Masuala ya Ukimwi kwa kuunda upya kamati hiyo na kuteua wajumbe wapya 16, ambao pia watakuwa ni wajumbe katika kamati nyingine za Kudumu za Bunge.

Kwa mujibu wa taarifa ya Kitengo cha Habari, Elimu na Mawasiliano cha Bunge jana kwa vyombo vya habari, mabadiliko hayo yamelenga kuwawezesha wabunge kujifunza na kujipatia uelewa na uzoefu zaidi katika kutekeleza shughuli mbalimbali za Kamati za Bunge, ambapo wabunge wote waliokuwa wajumbe wa Kamati ya Masuala ya Ukimwi awali, wamepangiwa Kamati zingine kwa nia ya kuboresha Utekelezaji wa majukumu ya kibunge.
“Msingi wa mabadiliko haya unatokana na Ibara ya 96 ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ya Mwaka 1977 inayolipa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania mamlaka ya kuunda Kamati za Bunge za namna mbalimbali kadri linavyoona inafaa, kwa ajili ya kurahisisha utekelezaji wa majukumu yake na Kanuni ya 116 (3) – (5) ya Kanuni za Kudumu za Bunge Toleo la Januari, 2016 inampa Spika mamlaka ya kuteua wabunge ili wawe wajumbe katika Kamati mbalimbali za Bunge, ikiwa ni pamoja na mamlaka ya kuongeza, kubadilisha au hata kupunguza idadi ya wajumbe katika Kamati za Kudumu za Bunge,” ilieleza taarifa ya Bunge.
Ilieleza kuwa kwa mujibu wa Waraka Na.5/2016 wa Spika kwa wabunge wote wa Oktoba 7, mwaka huu, mabadiliko haya yataanza kutekelezwa mara moja kuanzia mwezi huu ambao wajumbe husika watakutana kwa ajili ya kufanya uchaguzi wa viongozi wao na kuandaa ajenda za vikao vya kamati.
Taarifa hiyo iliwataja wajumbe wapya 16 wa Kamati ya Bunge ya Masuala ya Ukimwi na kamati zao nyingine katika mabano kuwa ni Asha Abdullah Juma (Katiba na Sheria), Daniel Mtuka (Sheria Ndogo), Dk Faustine Ndugulile (Huduma na Maendeleo ya Jamii), Dk Hadji Mponda (Mjumbe wa PAC), Dk Jasmine Bunga (Huduma na Maendeleo ya Jamii), Gibson Meiseyeki (Katiba na Sheria), Joseph Mhagama (Katiba na Sheria), Juliana Shonza (Mambo ya Nje, Ulinzi na Usalama).
Wengine ni Kemirembe Lwota (Ardhi, Maliasili na Utalii), Lucia Mlowe (Huduma na Maendeleo ya Jamii), Mary Muro (Miundombinu), Martha Mlata (Viwanda, Biashara na Mazingira), Masoud Abdalla Salim (Mambo ya Nje, Ulinzi na Usalama), Oscar Mukasa (Nishati na Madini), Stanslaus Nyongo (Viwanda, Biashara na Mazingira) na Yussuf Kaiza Makame (Nishati na Madini).
Waliohamishwa na kamati katika mabano ni Hassna Mwilima (Mambo ya Nje, Ulinzi na Usalama), Constantine Kanyasu (Uwekezaji wa Mitaji ya Umma(PIC), Muhammed Amour Muhammed (Uwekezaji wa Mitaji ya Umma (PIC), Sixtus Mapunda (Uwekezaji wa Mitaji ya Umma (PIC), Juma Kombo Hamad (Katiba na Sheria), Mattar Ali Salum (Kilimo, Mifugo na Maji), Savelina Mwijage (Huduma na Maendeleo ya Jamii), Khalifa Mohammed Issa (Utawala na Serikali za Mitaa), Abdallah Haji Ali (Hesabu za Serikali (PAC), Waitara Mwikabe (Utawala na Seikali za Mitaa), Khamis Yahya Machano (Mambo ya Nje, Ulinzi na Usalama) na Sikudhani Chikambo (Huduma na Maendeleo ya Jamii).
Wengine ni Zuberi Kuchauka (Miundombinu), Mgeni Jadi Kadika (Hesabu za Serikali za Mitaa (LAAC), Hussein Amar (Huduma na Maendeleo ya Jamii), Richard Mbogo (Hesabu za Serikali za Mitaa (LAAC), Grace Tendega (Huduma na Maendeleo ya Jamii), Elibariki Kingu (Sheria Ndogo), John Kadutu (Hesabu za Serikali za Mitaa (LAAC), Azza Hillal (Hesabu za Serikali za Mitaa (LAAC), Zaynab Vulu (Uwekezaji wa Mitaji ya Umma (PIC), John Heche (Nishati na Madini), Vuma Augustine (Uwekezaji wa Mitaji ya Umma (PIC) na Yahya Masare (Mambo ya Nje, Ulinzi na Usalama).